1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanariadha watatu wapigwa marufuku Kenya

22 Februari 2013

Baada ya kuenea uvumi kuhusu ripoti za wanariadha kutumia dawa za kusisimua misuli, wanariadha watatu wakenya wamepigwa marufuku baada ya kugunduliwa kutumia dawa hizo.

https://p.dw.com/p/17kJN
Kenya's Ezekiel Kemboi reacts on the track after winning the gold medal in the men's 3000m steeplechase final during the London 2012 Olympic Games at the Olympic Stadium August 5, 2012. REUTERS/Lucy Nicholson (BRITAIN - Tags: SPORT ATHLETICS OLYMPICS)
Olympia London 2012 3000 Meter HindernisPicha: Reuters

Wanariadha wa mbio za marathon Wilson Erupe Loyange na Nixon Kiplagat Cherutich watatumikia adhabu ya kutoshirikia katika mashindano yoyote kwa miaka miwili. Moses Kiptoo Kurgat amepigwa marufuku wka mwaka mmoja.

Mwanariadha wa nne Francis Kibiwott, ambaye alimaliza katika nafasi ya 45 katika ubingwa wa mbio za nusu marathon za mwaka wa 2007 nchini Italia aliondolewa shutuma baada ya kesi yake kutathminiwa na tume ya matibabu ya shirikisho la riadha duniani IAAF.

Kenya inayofahamika kutamba katika mbio za masafa ya kadri na marefu, imekuwa ikishutumiwa kufuatia ripoti za kuwepo matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku miongoni mwa mwanariadha wake maarufu. Katibu mkuu wa shirikisho la riadha Kenya David Okeyo amesema hawatawasamehe wanariadha watakaogundulika kutumia dawa hizo.

Schalke yalalamika kuhusu Drogba

Klabu ya Schalke 04 imewasilisha malalamishi kwa shirikisho la soka Ulaya UEFA kuhusiana na sare yao ya goli moja kwa moja na Galatasaray katika ligi ya Mabingwa kwa sababu ya kushiriki mchezaji Didier Drogba.

Schalke walitoka sare ya goli moja kwa moja na Galatasaray
Schalke walitoka sare ya goli moja kwa moja na GalatasarayPicha: Reuters

Drogba alicheza katika mchuano huo wa mkondo wa kwanza wa awamu ya mchujo, wiki moja baada ya shirikisho soka ulimwenguni FIFA kuruhusu uhamisho wake kutoka klabu ya Shanghai Shuenhua hadi klabu hiyo ya Uturuki.

Schalke imesema kuna shaka kuhusiana na uhalali wa Drogba katika Champions League, na imeitaka UEFA kuchunguza suala hilo la uhamisho wa Drogba. Shangha Shuenhua ililalamikia FIFA kwamba Drogba alikiuka mkataba wake. Mshambuliaji huyo wa Cote d'Ivoire ambaye alikuwa na mkataba hadi mwaka wa 2014, anadai kuwa hakuwa akilipwa mshahara wake. Kama FIFA itaamua kwa upande wa Shanghai, basi Drogba huenda akapigwa mafuruku na vikwazo vya kutofana ya uhamisho kuwekewa Galatasaray.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters

Mhariri: Josephat Charo