1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri watoa maoni juu ya Mubarak

Abdu Said Mtullya3 Agosti 2011

Kesi ya Mubarak ni mtihani mkubwa kwa Misri wasema wahariri wa magazeti ya Ujerumani

https://p.dw.com/p/12A0P
Wapinzani waliomng'oa Mubarak madarakani wataka apewe adhabu ya kitanziPicha: dapd

Aliekuwa Rais wa Misri Hosni Mubarak leo amefikishwa mahakamani akiwa katika kitanda cha hospitali kujibu mashtaka ya mauaji, rushwa na matumizi mabaya ya mamlaka.

Gazeti la Neue Osnabrücker linatoa maoni yake. Linasema kutokana na kesi hiyo Misri inakabiliwa na mtihani mgumu. Kwani Mahakama inaweza kumpa Mubarak adhabu ya kifo kutokana na mashtaka yanayomkabili. Ikiwa Mubarak atapatikana na hatia. Mhariri wa gazeti la Neue Osnabrücker pia anasema kwamba matokeo ya kesi ya Mubarak yatakuwa msingi wa kuijenga Misri mpya. Pia anatilia maanani kwamba mapinduzi ndiyo kwanza yameanza, na anauliza iwapo yataleta demokrasia nchini Misri.

Mhariri wa gazeti la Der neue Tag anatoa maoni juu ya matukio ya nchini Syria lakini kwa kutilia maanani uhusika wa jumuiya ya kimataifa.

Mhariri huyo anasema: "Vikwazo, hata vikiwa madhubuti havitautikisa utawala wa Rais Assad." Gazeti hilo pia linasema kuwa azimio dhaifu la Baraza la Usalama halitamzuia Rais Assad kuendeleza vita dhidi ya watu wake wenyewe.

Jee matumaini yatatoka wapi anauliza mhariri wa gazeti hilo? Umoja wa nchi za Kiarabu umekunja mikono na umejiweka mbali, nchi za magharibi zimezama katika jangwa la Libya na zinakwepa wazo la kujiingiza kijeshi nchini Syria. Kwa hiyo anasema mhariri ,mabadiliko yatakuja kutokea ndani ya Syria kwenyewe.

Gazeti la Nordbayerischer Kurier pia linayazungumzia matukio ya nchini Syria kwa kusema kwamba watawala wa nchi hiyo hawana haja ya kuwa na wasiwasi,na anaeleza ; Sababu ni kwamba Syria haitiliwi maanani sana kulinganisha na migogoro mingine. Pamoja na hayo nchi za Nato mpaka sasa bado hazijaweza kumwondoa Gaddafi. Hakuna anaetaka kujiingiza Syria kijeshi. Kwa hiyo watawala wa nchi hiyo hawana haja ya kuwa na wasiwasi.

Naye mhariri wa Nürnberger anazilaumu nchi za Umoja wa Ulaya kwa kuutumia mkuki butu dhidi ya utawala wa Assad. Mhariri huyo anasema nguvu za kijeshi zinatumika dhidi ya utawala wa Gaddafi. Lakini dhidi ya utawala wa Assad nchi za Ulaya zinatumia njia zilizozibika tokea mwanzo. Kuwawekea vikwazo watawala wa Syria ikiwa pamoja na kuwapiga marufuku kuingia katika nchi za Umoja wa Ulaya ni hatua inayostahili kupongezwa. Lakini hayo asilani hayatamzuia Rais Assad kuvitumia virafu dhidi ya watu wake.

Mwandishi/Mtullya abdu/Deutsche Zeitungen/

Mhariri/Abdul-Rahman