1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri watoa maoni juu ya mabadiliko katika chama cha FDP

Abdu Said Mtullya11 Mei 2011

Wahariri wa magazeti wasema chama cha FDP kinahitaji kupiga hatua ndefu zaidi ili kufanikiwa

https://p.dw.com/p/11DbN
Mwenyekiti Mtuele wa chama cha FDP Philipp Roesler (Kulia) akizungumza na waziri wa uchumi Rainer Brüderle pia wa FDPPicha: dapd

Chama cha Waliberali, cha FDP kilichomo katika serikali ya mseto nchini Ujerumani kimeanguka katika umaaruf na ndiyo sababu kwamba mabadiliko yamefanyika katika uongozi wa chama hicho.Jee mabadiliko hayo yatarejesha umaarufu wa chama hicho?

Mwenyekiti mteule wa chama hicho bwana Phillip Rösler amesema kuwa mabadiliko yaliyofanyika katika uongozi wa chama chake ni hatua ya kwanza katika juhudi za kuondokana na mgogoro unaokikabili chama chake.

Lakini wahariri wengi hawakubaliani na mtazamo wa bwana Rösler. Mhariri wa gazeti la Der neue Tag anasema mabadiliko yaliyofanyika hayaonekani kuwa ni mwanzo mpya. Mhariri huyo anasema kinachohitajika katika chama cha FDP sasa ni mabadiliko ya maudhui.

Gazeti la Flensburger Tageblatt linakubaliana na maoni ya mhariri wa gazeti la Der neue Tag kwa kusema kwamba, mabadiliko yaliyofanywa hayamwezeshi mwenyekiti mteule wa FDP bwana Rösler asimame kifua mbele. Moyo wa mabadiliko haukuonekana katika mageuzi yaliyoletwa. Kilichofanyika ni kubadilisha tu nyadhifa za viongozi.

Mhariri wa gazeti la Wetzlarer Neue Zeitung pia anasema kwamba mabadiliko yaliyofanyika katika chama cha FDP ni ishara potovu. Mhariri huyo anafafanua kwa kusema kwamba ikiwa mtu ameshindwa kulitekeleza jukumu fulani, basi anajaribu jingine linalotoa matumaini ya kumletea umaaruf. Lakini mtazamo huo hauendi sambamba na msingi wa utendaji kazi wa chama cha FDP. Na wala chama hicho hakitakuwa kinaenda sambamba na msingi huo, ikiwa baadhi ya wanasiasa fulani watachaguliwa kuwamo katika baraza la uongozi.

Naye mhariri wa gazeti la Leipziger anaeleza kuwa alichofanya mwenyekiti mteule wa chama cha FDP bwana Rösler katika kufanya mabadiliko siyo jawabu la matatizo ya chama chake. Bwana Rösler atalazimika kupiga hatua ndefu zaidi. Mhariri huyo anaeleza kuwa kwenye mkutano wake mkuu, mwishoni mwa wiki hii, chama cha FDP kitalazimika kuthibitisha kwamba bado kinahitajika. Haitatosha kwa mwenyekiti mpya kuonyesha tu kwamba yeye ni mtu mkarimu kuliko mwenyekiti wa hapo awali Guido Westerwelle.

Mwenyekiti mpya atalazimika kuyashughulikia masuala mengi zaidi ya kisiasa ili kuweza kufanikiwa. Lakini mhariri wa gazeti la Schwäbische anasema, kwa kufanya mabadiliko, Mwenyekiti mteule wa FDP , Rösler ameshapata sehemu ya mafanikio ya kwanza. Sasa chama cha FDP kinaweza kuyashughulikia masuala muhimu, baada ya kufanyika mabadiliko.Kwani chama hicho kimefikia hatua ambapo asilimia ya kura katika chaguzi siyo muhimu tena kuliko uhai wa chama !

Mwandishi/Mtullya Abdu/ Deutsche Zeitungen/

Mhariri/- Othman Miraj