1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi watumia mabomu yaliyopigwa marufuku Yemen

Admin.WagnerD20 Aprili 2017

Shirika la kimataifa la haki za binaadamu llimeshutumu matumizi ya mabomu yaliotegwa ardhini yanayofanywa na waasi wa madhehebu ya Shia Yemen ambayo yameuwa na kuwakata viungo mamia ya raia.

https://p.dw.com/p/2bd9P
Yemen Sanaa - Houthi Rebellen
Picha: Reuters/K. Abdullah

Katika repoti yao hiyo mpya iliyotolewa Alhamisi (20.03.4.2017) shirika hilo linasema waasi wanaojulikana kama Wahouthi ambao wanashirikiana na vikosi vya rais wa zamani wa nchi hiyo wametumia mabomu ya kutegwa ardhini katika majimbo yasiopunguwa sita tangu mwezi wa Machi mwaka 2015  wakati muungano uliokuwa ukiongozwa na Saudi Arabia ulipoanzisha mashambulizi yao dhidi yao.

Steve Goose mkurugenzi wa kitengo cha silaha katika shirika la haki za binaadamu la Human Rights Watch amesema Wahouthi na vikosi vya rais wa zamani Ali Abdullah Saleh wamekuwa wakikiuka marufuku ya mabomu yanayotegwa ardhini kwa kuwadhuru wananchi wa nchi hiyo.Ameongeza kusema kwamba Yemen ilipiga marufuku mabomu hayo ya kutegwa ardhini miongo miwili iliopita.

Muungano unaoongozwa na Saudi Arabia wenye kujumuisha nchi kadhaa za Kiarabu za mdhehebu ya Sunni umekuwa ukifanya mashambulizi ya kuwan'gowa Wahouthi ambao waliteka mji mkuu wa Yemen na maeneo mengine ya nchi hiyo hapo mwaka 2014 na kuilazimisha serikali iliokuwa ikitambuliwa kimataifa kuikimbia nchi hiyo.

Kuwajibishwa wahusika

Yemen Sanaa - Menschenmengen bei Essensausgabe
Wananchi wa Yemen wakigombania msaada wa chakula mjini Sanaa.Picha: Reuters/K. Abdullah

Kristine Beckerle mtafiti wa Shirika la Human Rights Watch amesema shirika lake hilo limegunduwa aina mbili za mabomu yanayotegwa ardhini yanayokusudia kuwadhuru binaadamu ambayo huko nyuma hayakuwahi kurepotiwa nchini Yemen juu ya kwamba amesema sio tu vikosi vya Wahouthi na Saleh vyenye kuyatumia mabomu hayo bali pia muungano unaoongozwa na Saudi Arabia umekuwa ukitumia mabomu hayo.

 Beckele amesema "Sio tu Wahouthi wanaotumia silaha hizo zilizopigwa marufuku, Wasaudi wanatumia mabomu mtawanyo.Hayo pia yamepigwa marufuku.Kwa hiyo kile tunachosema ni kwamba kuna ukosefu kabisa wa taarifa juu ya kile wanachotenda vikosi hivyo.Baada ya miaka mitatu ya vita hivyo wakati umefika kuwajibisha wahusika, kuchunguza na kurepoti hadharani juu ya kile kinachotokea."

Umoja wa Mataifa leo hii pia umeonya kuhusu kuongezeka kwa matumizi hayo ya mabomu ya kutegwa ardhini na ukosefu wa chakula,madawa na maji nchini kote Yemen.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AP

Mhariri : Iddi Ssessanga