1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi wa LRA waua watu 200 DRC

Jane Nyingi29 Desemba 2008

Kiasi cha watu 200 wameauwa na waasi wa kundi la Lords Resistance Army kufuatia mashambuilizi ya siku tatu kaskazini mashariki mwa jamuhuri ya kidemocrasia ya Congo.

https://p.dw.com/p/GOq1
Wakimbizi katika eneo la Mashariki mwa Kongo ambao sasa wanakabiliwa na hatari ya mashambulizi ya waasi wa LRA wa UgandaPicha: AP

Yamkini watoto 20 na idadi ya watu wasiojulikana walitekwa nyara na waasi hao wa LRA wakati wa mashambulizi hayo.


Kwa mujibu wa ripoti za shirika la umoja wa mataifa linalotoa huduma za kiutu –OCHA mauji hayo yalitekelezwa kati ya tarehe 25 na 27 mwezi huu katika vijiji vya Faradje,Doruma na gurba. Waasi hao walikuwa katika pilka pilka za kutoroka mashambulizi dhidi yao yaliyooanzishwa wiki mbili zilizopita na vikosi vinavyoongozwa na Uganda.


Hata hivyo waliojipata taambani ni wenyeji wa vijiji hivyo vilivyo kaskazini mashariki mwa jamuhuri ya kidemocrasia ya congo.Miongoni mwa waliouawa 40 ni kutoka kijiji cha Faradhe, 89 kutoka Doruma na wenyeji 60 wa kijiji cha Gurba.


Majeshi ya Uganda, Jamuhuri ya kidemocrasia ya congo na Kusini mwa Sudan yalianzisha mashambulizi katika kambi za waasi wa LRA kaskazini mashariki mwa jamuhuri ya kidemocrasia ya Congo tarehe 14 mwezi huu baada ya kiongozi wao Joseph Kony kukataa kwa mara nyingine kutoa saini makataba wa amani ,ili kusitisha maasi dhidi ya serikali ya Uganda.


Kony amesema amesita kutia saini makubaliano hayo yaliyokamilishwa mwezi aprili mwaka huu kutokana na hati iliyotolewa na mahakama ya kimataifa dhidi ya uhalifu, ya kutiwa nguvuni kwake na pia viongozi wakuu wa kundi hilo la waasi la LRA na mahakama hiyo.


Licha ya mashambuluzi ya mabomu na vikosi hivyo vinavyoongozwa na Uganda, katika kambi za waasi hao wa LRA, hajaweza kujua aliko kony. Kiongozi huyo wa waasi anafahamika kwa kuwateka nyara wanawake na watoto ambapo kisha baadaye huwalazimisha watoto kujiunga na kundi lake la waasi.

Hata hivyo Kony amekanusha kuwa waasi wa LRA ndio waliotekeleza mauaji hayo ya hivi majuzi na kukinyooshea kidole cha lawama majeshi ya Uganda. Kupitia kwa msemaji wake Kony aliyashtumu vikali mauji hayo dhidi ya wenyeji wa kaskazini mashariki mwa Congo.

Waasi hao wa LRA kutoka nchini Uganda wameshtumiwa kwa kuwabaka wanawake na kuhusika katika mauji ya halaiki kufuatia mashambulizi ya miongo miwili kaskazini mwa Uganda kati yao na majeshi ya Uganda. karibu watu millioni mbili pia wamewachwa bila makao.


Waziri wa maswala ya kigeni nchini Uganda Okello Oryem amesema taarifa za kijasusi walizonazo ni kuwa waasi hao wa LRA sio zaidi ya elfu mbili na waliojihami si zaidi ya mia 700.











►◄