Volcano yazidi kumwaga jivu angani Ulaya
17 Aprili 2010Eneo kubwa la bara la Ulaya limeendelea kuwa lisiloweza kupitika kwa njia ya anga wakati wingu kubwa la majivu kutoka katika mlipuko wa volcano nchini Iceland kuendelea kusambaa hadi leo Jumamosi. Viwanja vyote 16 vya ndege nchini Ujerumani vimefungwa, wakati viwanja vya ndege mjini Paris , havitafunguliwa hadi mchana leo Jumamosi. Brian Flynn, naibu mkuu wa udhibiti wa usafiri wa anga katika bara la Ulaya , ambalo ni shirika linaloratibu usafiri wa anga katika mataifa 40, amesema kuwa tukio hili ni la kwanza kuvuruga safari za anga katika historia ya usafiri katika bara la Ulaya. Majivu hayo ni hatari kwa injini za ndege pamoja na kuzuwia marubani kuweza kuona waendako. Wingu la majivu limesambaa kutoka eneo la bahari ya Atlantic hadi Moscow na kutoka katika eneo la Arctic hadi Austria na Bulgaria kusini mwa bara la Ulaya. Wakati huo huo, baraza la usalama la umoja wa mataifa limesema kuwa limefuta safari yake katika jamhuri ya kidemokrasi ya Congo, kutokana na sababu za mvurugiko wa safari za anga katika bara la Ulaya.