1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa EuroMed7 wako tayari kwa vikwazo kwa Uturuki

Tatu Karema
11 Septemba 2020

Viongozi wa mataifa saba yanayopakana na bahari ya Mediterenia EuroMed7 wamesema wako tayari kuunga mkono vikwazo vya EU dhidi ya Uturuki iwapo itapuuza mazungumzo ya mvutano katika eneo la Mashariki mwa bahari hiyo

https://p.dw.com/p/3iJHw
Libanon Beirut Pressekonferenz Emmanuel Macron
Picha: picture-alliance/AP Images/G. Fuentes

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron Alhamisi alikuwa mwenyeji  wa viongozi wa mataifa mengine sita ya Umoja wa Ulaya yanayojumuisha Ugiriki ambayo ni mpinzani wa Uturuki katika kanda hiyo kwa mkutano katika kisiwa cha Ufaransa cha Corsica.

Akionesha ghadhabu yake dhidi ya Uturuki chini ya uongozi wa rais Recep Tayyip Erdogan, Macron alisema kuwa taifa hilo mshirika wajumuiya ya kujihami ya NATO sio mshirika tena katika eneo la Mashariki mwa bahari ya Mediterenia na kwamba raia wake wanastahili mambo tofauti kinyume na vile serikali hiyo inavyofanya kwa sasa.

Baada ya mkutano huo na viongozi wa Italia, Malta, Ureno, Uhispania, Ugiriki na Cyprus katika mji wa pwani wa kitalii nje kidogo ya mji mkuu wa jimbo la Corsica, Ajaccio, Macron alitumia maneno yasiokuwa na ukali na kusema viongozi hao walitaka kurejelea mazungumzo na Uturuki kwa ''nia njema.''

Uwezekano wa Uturuki kuwekewa vikwazo 

Lakini taarifa ya mwisho ya viongozi hao ilionesha wazi kuwa vikwazo ni suala linalozingatiwa iwapao Uturuki itashindwa kumaliza ''vitendo vyake vya uchokozi.'' Taarifa hiyo ilisema kuwa viongozi hao wanasikitika kuwa Uturuki haijajibu miito ya mara kwa mara ya Umoja wa Ulaya kusitisha shughuli zake haramu zinazolemea upande mmoja katika eneo la Mashariki mwa bahari ya Mediterenia na bahari ya Aegean.

Kupitia taarifa hiyo, viongozi hao wameendelea kusema wanadumisha msimamo wao kwamba kwa kukosekana kwa ufanisi katika kuishirikisha Uturuki katika mazungumzo na iwapo haitatamatisha vitendo vyake haramu basi Umoja wa Ulaya uko tayari kutengeneza orodha ya vikwazo vikali zaidi ambavyo huenda vikajadiliwa katika mkutano wa baraza la Umoja huo mnamo Septemba 24-25.

Matokeo ya mkutano huo wa jana yanatuma ujumbe wazi wa uungwaji mkono kwa Ugiriki na Cyprus katika mkwamo unaoongezeka na Uturuki kuhusiana na maliasili ya gesi ya mafuta pamoja na ushawishi wa jeshi la majini katika eneo la Mashariki mwa Mediterenia ambao umezusha hofu ya mzozo.