1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vifo vya Covid-19 vyapindukia 500,000 Marekani

Bruce Amani
23 Februari 2021

Rais Joe Biden ameamuru bendera kupeperushwa nusu mlingoti baada ya idadi ya vifo vya Marekani kutokana na Covid-19 kupindukia 500,000. Biden ameonya idadi hiyo huenda ikaongezeka kama hatua zaidi hazitachukuliwa

https://p.dw.com/p/3pjNX
USA I Biden Rede über Corona-Tote
Picha: Jonathan Ernst/REUTERS

Akilihutubia taifa kupitia televisheni, Biden aliwaomba Wamarekani wote kuwakumbuka wale wote waliofariki dunia na waliowapoteza wapendwa wao. Amewahimiza Waamrekani kuchukua hatua, kuwa waangalifu, kuvaa barakoa, kutosogeleana na kupewa chanjo. Awali, bendera zilipepea nusu mlingoti katika Ikulu ya White House na majengo mengine ya serikali kote nchini pamoja na balozi zake kote duniani.

Biden ameonya kuwa idadi ya vifo Marekani huenda ikapimndukia 600,000. Lakini dalili pia zinaonekana kuwa hatua zimepigwa nchini Marekani na kwingineko duniani, huku idadi ya maambukizi ikipungua kwa kiasi kikubwa na utoaji wa chanjo ukiongezeka.

Nchini Uingereza, Waziri Mkuu Boris Johnson ametangaza mpango wa kuanza kulegeza taratibu na kwa tahadhari kubwa vikwazo nchini humo ili kurejesha maisha ya kawaida ifikapo mwishoni mwa Juni. Hatua ya kwanza itakuwa ni kurejea shuleni kwa wanafunzi kuanzia Machi 8.

Wakati huo huo, mamia kwa maelfu ya wanafunzi wa Ujerumani walirejea jana shuleni kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miezi miwili. Hata hivyo, kuanza kutekelezwa kwa uamuzi huo jana, kulisadifiana na kutolewa kwa takwimu mpya ambazo zinaonesha kuwa idadi ya maambukizo mapya imepanda kwenye baadhi ya maeneo ya nchi.

AFP, AP, Reuters, DPA