1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UNHCR itazidisha huduma zake Kivu ya kaskazini

Oummilkheir16 Desemba 2007
https://p.dw.com/p/CcLC

Goma:

Mwenyekiti wa halmashauri kuu ya Umoja wa mataifa inayowashughulikia wakimbizi UNHCR,Antonio Guterres amesikitishwa na kile alichokiiita “msiba unaowakumba binaadam” katika jimbo la mashariki la Kivu ya kaskazini-katika jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo.Katika mkutano pamoja na waandishi wa habari hii leo mjini Goma,Antonio Guterres amesema watazidisha shughuli zao Kivu ya kaskazini kwa ushirikiano pamoja na mashirika mengineyo,ili kuimarisha hali ya maisha katika kambi za wakimbizi.”Amani ni sharti la kwanza muhimu ili kusitisha msiba huu” amesisitiza mwenyekiti huyo wa shirika la Umoja wa mataifa la UNHCR.Watu wanaokadiriwa kufikia laki nane wanaranda randa tangu mwishoni mwa mwezi wa Agosti uliopota, wakiyapa kisogo mapigano kati ya vikosi vya serikali na waasi katika eneo hilo la mashariki ya jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo.Antonio Guterres aliyekua katika ziara ya siku tatu Kivu ya Kaskazini, anatazamiwa kurejea Kinshasa hii leo kwa mazungumzo pamoja na rais Joseph Kabila,kabla ya kuondoka jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo baadae kesho usiku.