1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umwagaji damu waendelea Ukraine

20 Februari 2014

Watu 21 wameuwawa Alhamisi (20.02.2014)katika mapambano mapya kati ya polisi wa kutuliza fujo na waandamanaji mjini Kiev,Ukraine wakati mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya wakikutana na Rais Vikctor Yanukovich.

https://p.dw.com/p/1BByy
Mwanamke abwaga kilio wakati waandamanaji wakiweka maiti kwenye machela Kiev.(20.02.2014).
Mwanamke abwaga kilio wakati waandamanaji wakiweka maiti kwenye machela Kiev.(20.02.2014).Picha: Reuters

Mapambano mapya yameibuka kati ya polisi wa kutuliza fujo na waandamanaji leo hii katika mji mkuu wa Ukraine, Kiev, na kutibua mpango tete wa suluhu wakati mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya wakikutana na Rais Vikctor Yanukovich kujaribu kutafuta ufumbuzi wa mzozo huo.

Mapambano hayo ya leo yamezuka wakati waandamanaji waliojifunukia nyuso walipowarushia polisi wa kutuliza fujo mabomu ya petroli na mawe katika uwanja wa Uhuru mjini Kiev ambacho ni kitovu cha mzozo wa kisiasa wa jimbo hilo la zamani la Muungano wa Kisovieti.

Waanadamanaji hao walifanikiwa kuwarudisha nyuma polisi kwa kama mita 200 na na kuweza kuudhubiti tena uwanja huo wote ambao waanadamanaji wanaopinga serikali walikuwa wakiukalia kwa mabavu tokea mwezi wa Novemba mwaka jana.

Polisi ilitumia risasi za mpira kujaribu kuzima shambulio la waandamanaji hao na imedai kwamba mashambuliaji wa kuvizia amewajeruhi polisi 20 kwa kuwafyetulia risasi za moto kutoka kwenye jengo linaloelekezana na uwanja huo ulipgubikwa na moshi.

Suluhu yatibuka

Mapambano hayo yametibua suluhu waliokubaliana kati ya Rais Viktor Yanukovych na viongozi wa upinzani masaa machache kabla kufuatia umwagaji damu uliogharimu maisha ya takriban watu 28 katika kipindi cha siku mbili.

Waandamanaji wakiomboleza mbele ya maiti zilizofunikwa mablangeti Kiev.(20.02.2014).
Waandamanaji wakiomboleza mbele ya maiti zilizofunikwa mablangeti Kiev.(20.02.2014).Picha: Reuters

Taarifa fupi iliyochapishwa kwenye wovuti wa ofisi ya rais hapo jana usiku haikutowa maelezo suluhu hiyo inamaanisha nini au itatekelezwa vipi na wala haikufafanuwa mazungumzo yatafanyika vipi na pia haikodokeza iwapo yatakuwa tafauti na mikutano iliofanyika huko nyuma kati ya rais na viongozi wa upinzani.

Shinikizo la kimataifa

Mbinu za kisiasa na za kidiploamasia zimekuwa zikiendelezwa ambapo pande zote mbili Urusi na mataifa ya magharibi zimekuwa mbioni kujenga ushawishi wao kwa nchi hiyo. Mawaziri watatu wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya kutoka Ujerumani,Ufaransa na Poland wako Kiev leo hii kuzungumza na pande mbili zinazohasimiana kabla ya mkutano wao dharura wa Umoja wa Ulaya mjini Brussels baadae leo hii kufikiria hatua za kuchukuwa dhidi ya wale waliohusika na umwagaji damu wa hivi karibuni nchini humo.

Waandamanaji wakiwa na majeruhi Kiev.(20.02.2014).
Waandamanaji wakiwa na majeruhi Kiev.(20.02.2014).Picha: Reuters

Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov amezungumza na waziri mwenzake wa Ujerumani Frank -Walter Steinmeier na kumtaka kutumia mawasiliano yake ya karibu na ya kila siku na upinzani wa Ukraine kutafuta ufumbuzi wa mzozo huo.

Wizara ya mambo ya nje ya Urusi imeelezea ghasia hizo kuwa ni jaraibio la mapinduzi na hata kutumia neno "mapinduzi ya kibaguzi" kwa kuyafananisha na kusimama kwa utawala wa Manazi nchini Ujerumani hapo mwaka 1933. Wizara hiyo imesema Urusi itatumia ushawishi wake wote kurudisha amani na utulivu nchini humo.

Rais Barack Obama wa Marekani pia amelaani umwagaji damu uliotokea na kuonya kwamba itaichukulia hatua nchi hiyo iwapo hali hiyo itaendelea ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kujiuga na Umoja wa Ulaya kuiwekea vikwazo Ukraine.

Mwandishi: Mohamed Dahman/AFP/AP

Mhariri: Mohammed Khelef