1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waaandishi wa habari 110 wauawa wakiwa kazini

29 Desemba 2015

Jumla ya waandishi wa habari 110, waliuawa duniani kote katika kipindi cha mwaka 2015, hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa ripoti ya shirika la maripota wasio na mipaka (RSF) .

https://p.dw.com/p/1HUwp
Symbolbild Pressefreiheit
Picha ikionyesha ukatili dhidi ya waandishi wa habariPicha: picture-alliance/dpa/I. Langsdon

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya RSF waandishi wa habari 67 waliuawa wakati wakitekeleza wajibu wao wa kazi katika kipindi cha mwaka huu, na wengine 43 waliuawa katika mazingira ambayo hayajaeleweka. Waandishi wengine wa habari 27 wasio na taaluma kamili ya uandishi wa habari na wafanyakazi wengine 7 kutoka katika vyombo vya habari nao pia waliuawa.

Idadi hiyo kubwa ya vifo vya waandishi wa habari imeelezwa kuchangiwa zaidi na ukatili unaofanywa dhidi ya waandishi hao wa habari wakati wanapokuwa wakitekeleza wajibu wao wa kazi. Hali hii inaashiria kushindwa kuchukua hatua za kuwalinda waandishi wa habari imesema ripoti hiyo na kuutaka Umoja wa Mataifa kuchukua hatua. Ripoti hiyo inazidi kutoa mwanga juu ya kuongezeka kwa matukio ya mauaji dhidi ya waandishi wa habari yanayofanywa na makundi yasiyokuwa na mahusiano na serikali kama vile makundi ya itikadi kali mfano kundi la Dola la Kiisilamu.

Reporter Ohne Grenzen Iran Aktivist Protest
Waandishi wasiokuwa na mipaka wakionesha picha hiyo kupinga kukamatwa kwa waandishi habariPicha: Loic Venance/AFP/GettyImages

"Kuna umuhimu sasa wa kuandaliwa utaratibu wa kuwa na sheria ya kimataifa itakayowalinda waandishi wa habari" alisema Christophe Deloire ambaye ni katibu mkuu wa shirika la maripota wasio na mipaka. Idadi ya waandishi wa habari 110 waliouawa mwaka huu inaashiria kuwa kuna haja ya kuchukua hatua za haraka za kukabiliana na vitendo hivyo. Mwakilishi maalumu kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atakaye shughulikia kulindwa kwa waandishi wa habari wanapokuwa wanatekeleza wajibu wao anapaswa ateuliwe bila kuchelewa," ameongeza kusema Deloire.

Kwa mujibu wa shirika hilo la maripota wasio na mipaka lenye makao yake jijini Paris Ufaransa idadi ya vifo 67 inafanya idadi ya waandishi wa habari 787 waliouawa katika mauaji ya kupangwa au wakati wakitekeleza wajibu wao tangu mwaka 2005. Kwa mwaka 2014, kulikuwa na mauaji ya aina hiyo 66 dhidi ya waandishi wa habari.

Mataifa yenye migogoro ni kitisho kwa waandishi wa habari

Mataifa yanayokabiliwa na migogoro kama vile Iraq na Syria yameonekanakuwa ni mataifa yaliyokuwa ya hatari zaidi kwa waandishi wa habari kwa mwaka huu. Ufaransa imechukua nafasi ya tatu katika orodha hiyo kufuatia tukio la kuuawa waandishi wa habari wanane wa jarida la tashtit la Charlie Hebdo nchini humo mwezi January mwaka huu.

Tukio la mauaji ya waandishi hao wa habari lilikuwa ni tukio ambalo halijawahi kutokea katika taifa hilo katika kipindi cha nyuma na waandishi wa habari wa jarida hilo tangu hapo wamekuwa wakiishi chini ya uangalizi na baadhi yao wamekuwa wakibadilisha maeneo yao ya makazi.

Türkei Beerdigung Naji Jerf
Waandishi habari wakibeba picha za mwenzao aliyeuwawa nchini Uturuki Naji JerfPicha: Getty Images/AFP/Str

Nchini Syria mji wa kasikazini wa Allepo nao pia umetajwa kuwa miongoni mwa miji ambayo imekuwa kitisho kwa maisha ya waandishi wa habari.

Hali hii inaashiria kuwa waandishi wa habari wako katika hatari ya kupoteza maisha wanapokuwa wanatekeleza wajibu wao wa kazi kutokana na matukio ya kukamatwa na kufanywa mateka na makundi ya itikadi kali kama vile kundi la dola la kiisilamu .

Miongoni mwa waliouawa nchini Syria ni mwandishi wahabari wa kujitegemea kutoka nchini Japan, Kenji Goto ambaye aliuawa na kundi la dola la Kiislamu.

Ripoti ya shirika hilo la maripota wasio na mipaka imeitaja pia India ambako waandishi wa habari tisa waliuawa tangu mwanzoni mwaka 2015, baadhi yao kwa kufichua taarifa za mauaji yaliyopangwa na kuhusihwa kwa mauaji hayo na wanasiasa.

Mwandishi: Isaac Gamba/ AFPE

Mhariri: Iddi Ssessanga