1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa waipa DRC siku mbili

Saumu Mwasimba
6 Juni 2017

Umoja wa Mataifa umeitaka serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuridhia wito wake wa kufanya uchunguzi dhidi ya mauaji ya Kasai ndani ya siku mbili vyenginevyo hatua zaidi zichukuliwe.

https://p.dw.com/p/2eBCb
Angola flüchtchtlings Kinder aus Kongo
Picha: UNICEF/N. Wieland

Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Zeid Raad al-Hussein, amesema serikali ya Rais Joseph Kabila inapaswa kuendesha kwa pamoja uchunguzi kuhusu vurugu za mkoa huo, la sivyo utafanyika uchunguzi wa lazima wa kimataifa kuhusu haki za binadamu.

Zeid ametoa kauli hiyo mbele ya kikao cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mjini Geneva unaoendelea sasa.

Zeid amesema hali mbaya iliyopo mkoa wa Kasai inaendelea kuwa mbaya zaidi na kuenea katika mikoa mingine na nje ya mipaka ya Kongo na kuingia Angola.

Kadhalika, mkuu huyo wa Kamisheni ya Haki za Binaadamu ya Umoja wa Mataifa ameweka wazi kwamba endapo hatopokea majibu mwafaka kutoka serikali ya Kongo kuhusiana suala la kuridhia uchunguzi wa pamoja kufikia tarehe 8 Juni nitasistiza kuundwe tume maalum ya kimataifa ya uchunguzi kwa ajili ya watu wa Kasai.