1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa waadhimisha miaka 70 tangu kuundwa

23 Oktoba 2015

Umoja wa Mataifa unaadhimisha mwaka wa 70 tangu uundwe lakini pana wasi wasi iwapo taasisi hiyo imelitimiza jukumu lake kuu - kulinda amani ya dunia

https://p.dw.com/p/1GtNG
Picha: picture-alliance/AA/C. Ozdel

Katika kuadhimisha mwaka wa 70 tangu kuundwa kwake ,Umoja wa Mataifa unakabiliwa na changamoto kubwa. Mashaka juu ya shirika hilo yanazidi kuwa makubwa.

Umoja wa mataifa unaadhimisha miaka 70 ya historia yake wakati ambapo dunia inashuhudia ugaidi unaofanywa na makundi ya itikadi kali,vitisho vya kufanya mashambulio kwa silaha za nyuklia vinavyotolewa na Korea ya Kaskazini na wakati ambapo Mashariki ya Kati kwa mara nyingine imo katika hatari ya kuzama katika vurumani kubwa .

Hiyo ni sehemu ndogo tu ya migogoro inayowafanya watu wawe na hofu kwamba nguzo iliyokuwa inaishikilia dunia inatenguka. Lakini palikuwa na haja ya kuwa na mlinda amani wa dunia kama Umoja wa Mataifa?

Maadhimisho ya miaka 70 tangu kuundwa kwa Umoja huo, yamegubikwa na lawama. Shirika hilo linazingatiwa, zaidi , kuwa la ubadhirifu na udhaifu katika kupitisha maamuzi kuliko kuwa la kulinda amani.

Shirika hilo linazingatiwa kuwa chama cha porojo

Mara nyingi watu wanasema makao makuu ya Umoja wa Mataifa, mjini New York yako mbali sana na sehemu za vita na migogoro. Lawama dhidi ya Umoja wa Mataifa zimeongezeka kutokana na vita vya nchini Syria.

Katibu Mkuu wa Shirika la kutetea haki za binadamu,Amnesty International Salil Shetty
Katibu Mkuu wa Shirika la kutetea haki za binadamu,Amnesty International Salil ShettyPicha: dapd

Mashirika ya misaada 21,mnamo mwezi ya Machi mwaka huu, yaliulaumu Umoja wa Mataifa kwa kushidwa kabisa kuyatimiza majukumu yake.

Katibu Mkuu wa shirika la kutetea haki za binadamu duniani, Amnesty International Salil Shetty ameulaumu Umoja wa Mataifa kwa namna unavyoushughulikia mgogoro wa wakimbizi.Amesema Umoja wa Mataifa umetia aibu katika suala la wakimbizi.

Lakini aliekuwa balozi wa Ujerumani kwenye Umoja wa Mataifa Hanns Schumacher amesema ni wanachama wa Umoja huo wanaopaswa kulaumiwa . Balozi huyo mstaafu amesema Umoja wa mataifa mara nyingi unashindwa kuitatua migogoro kutokana na baadhi ya wanachama kukataa kushirikiana na Umoja huo. Hata hivyo balozi Schumacher ametilia maanani umuhimu wa kazi inayofanywa na Shirika hilo duniani.

Balozi Schumacher amesema Umoja wa Mataifa unatoa mchango maalumu katika dunia hii ya utandawazi. Hatahivyo ameleeza kuwa haina maana kwamba makosa hayafanyiki.

Balozi huyo mstaafu ametilia maanani kwamba baadhi ya matatizo kama vile maradhi ya miripuko yanaweza kudhibitiwa kwa juhudi za pamoja za wanachama wa Umoja wa Mataifa. Lakini ameukosoa mfumo wa Baraza la Usalama ambapo kila mwanachama wa kudumu anao uwezo wa kuzuia maamuzi yasiyompendeza.

Mwandishi:Bosen,Ralf

Mfasiri:Mtullya Abdu.

Mhariri:Josephat Charo