Ujerumani yaadhimisha Siku ya Muungano
3 Oktoba 2011Kansela Angela Merkel na Rais Christian Wulff wa Ujerumani ni miongoni mwa viongozi mashahuri wanaohudhuria sherehe kuu za kuadhimisha muungano wa Ujerumani aambazo mwaka huu zinafanywa katika mji mkuu wa zamani wa Ujerumani ya Magharibi, Bonn. Sherehe za muungano wa Ujerumani zimefunguliwa rasmi leo hii katika mji wa Bonn kwa misa ya ekumeni iliyohudhuriwa na takribana wageni elfu moja chini ya ulinzi mkali. Miongoni mwa wageni mashuhuri ni Kansela Angela Merkel, Rais Christian Wulff, Rais wa Bunge la Ujerumani Norbert Lammert.
Baadae sherehe za muungano wa Ujerumani zitaendelea katika bunge la zamani la mjini Bonn ambako Rais wa Baraza la serikali za mikoa-Bundesrat, Hannelore Kraft alie pia waziri mkuu wa jimbo la North-Rhine Westphalia-(NRW) na Rais wa Mahakama ya Katiba ya Ujerumani, Andreas Voßkuhle watatoa hotuba kuu. Sherehe za miaka 21 ya muungano wa Ujerumani zinafanywa pamoja na sherehe za kuadhimisha miaka 65 ya kuundwa jimbo la North-Rhine Westfalia na zimeanza tangu siku ya jumamosi. Mamia ya watu wanasongana katika maeneo maalum yaliyotengwa kwa sherehe hizo ambako majimbo 16 ya Ujerumani yanawakilishwa sawa na idara mbali mbali za serikali ya jimbo la Northrhine Westphalia na mji wa Bonn.
Deutsche Welle pia kama sehemu ya sherehe za muungano wa Ujerumani hapo jana, ilikuwa na tafrija maalum ambapo kwa mara ya kumi imetoa "Zawadi ya Muungano". Mshindi hutunukiwa zawadi hiyo kama kitambulisho cha mchango na jitahada zake za kuzileta karibu zaidi pande mbili za Ujerumani. Tangu mwezi wa Septemba watu binafsi na mashirika yameshindana kuchaguliwa na jopo huru la majaji chini ya uenyekiti wa Joachim Gauck. Washindi hao wamechaguliwa chini ya kundi la vijana, utamaduni na binadamu. Kutoka kila kundi, wamepatikana washindi wawili na wamegawana zawadi hiyo ya muungano iliyo na thamani ya Euro 15,000.
Kabla ya sherehe za leo kufunguliwa rasmi, Kansela Merkel aliekulia Ujerumani ya Mashariki alisema, bado kuna tofauti kubwa na hasa katika soko la ajira ambapo ukosefu wa ajira ni mkubwa zaidi upande wa mashariki. Katika hotuba yake ya kila wiki kwenye mtandao, Merkel amesema hata hivyo kuna mengi ya kufuarhia muungano huo upya. Ujerumani ya Magharibi na Ujerumani ya Mashariki ya kikomunisti ziliungana tarehe 3 Oktoba mwaka 1990, yaani chini ya miezi 11 baada ya Ukuta wa Berlin kufunguliwa.
Mwandishi: Martin,Prema
Mhariri:Othman, Miraji