1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhispania yalenga kuandikisha historia

30 Juni 2012

Uhispania inadhamiria kuandikisha historia katika dimba la UEFA EURO 2012 katika fainali ya kesho Jumapili, lakini itapambana na kikosi cha Italia ambacho hakina lolote la kujuta.

https://p.dw.com/p/15Of1
Spain's players celebrate after defeating Portugal in their Euro 2012 semi-final soccer match at the Donbass Arena in Donetsk, June 27, 2012. REUTERS/Charles Platiau (UKRAINE - Tags: SPORT SOCCER)
UEFA EURO 2012 Halbfinale Portugal vs Spanien JUBELPicha: Reuters

Safari ya Uhispania kufikia fainali ya kesho mjini Kiev inaendeleza mbinu ambayo timu hiyo imetawala ulimwengu wa soka tangu iliposhinda kombe la UEFA EURO 2008 mjini Vienna, Austria. Uhispania waliongeza taji la ulimwengu mnamo mwaka 2010 na ushindi wa kesho jumapili utakuwa wa kwanza kushinda mataji matatu makuu mfululizo. Na pia watakuwa wa kwanza kutwaa taji la UEFA EURO mara mbili mfululizo, na kufikia rekodi ya Ujerumani ya jumla ya mataji matau katika kinyang'anyiro cha kimataifa.

Italy, hata hivyo, haitakuwa rahisi kushindwa, na Cesare Prandelli amebadilisha msimamo wake kabla ya mchuano huo wa kuamua. Anasema Uhispania ndio mabingwa wa ulimwengu na Ulaya na ni mfano wka kila mtu. Lakini wao wameimarika na hawafai kuwaogopa. Ni lazima wawe na nguvu za kuwakabili kwa mawazo na ubora wa mchezo.

Mario Balotelli ni moto wa kuotea mbali kwa mashambulizi ya Italia
Mario Balotelli ni moto wa kuotea mbali kwa mashambulizi ya ItaliaPicha: AP

Prandelli, ambaye alichukua usukani wa timu ya taifa Azurri kutoka kwa Marcello Lippi baada ya kushindwa katika kombe la dunia 2010, anajaribu kuifikisha Italy katika ushindi wao wa pili wa taji la Ulaya tangu mwaka wa 1968. Mawazo yoyote ya kuubadili mchezo wake ili kukabiliana na mfumo wa Uhispania huenda yakapumzishwa kutokana na kushindwa Ujerumani katika nusu fainali wakati Joachim Löw alipoubadili mfumo wake wa ushindi dhidi ya Italy na kushindwa magoli mawili kwa moja.

Timu hizo mbili tayari zimekutana katika awamu ya makundi na kutoka sare ya goli moja kwa moja, ambapo Antonio di Natale ndiye mchezaji pekee aliyefunga dhidi ya Uhispania katika dimba hili. Uhispania kufika katika fainali ni kitu kilichotarajiwa, ijapokuwa kitu cha pekee kilichoshangaza katika timu hiyo tu ilikuwa uamuzi wa Vicente del Bosque kucheza bila mshambuliaji.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 61 alimchezesha kiungo Cesc Fabregas katika safu ya mashambulizi dhidi ya Italia, na akarejea kwa Fernando Torres kwa mechi mbili zilizofuata. Kisha Fabregas tena katika robo fainali dhidi ya Ufaransa na akasababisha mshangao mwingine tena katika nusu fainali dhidi ya Ureno alipompa fursa Alvaro Negredo. Baada ya kumwondoa uwanjani Negredo mapema katika kipindi cha pili, inaonekana del Bosque ataanza na Torres au Fabregas dhidi ya Italy katika fainali. Katika lango nahodha Iker Casillas anahitaji tu ushindi mmoja na kuwa mchezaji wa kwanza kufikia kiwango cha kushinda mechi 100 za kimataifa.

Mbele yake ni Alvaro Arbeloa, Sergio Ramos, Gerard Pique na Jordi Alaba katika safu ya ulinzi ambayo haijafungwa goli katika mechi tisa mfululizo za awamu ya muondowano katika dimba la UEFA EURO na kombe la dunia tangu mwaka wa 2006. Xabi Alonso na Sergio Busquests watakuwa katika safu ya ulinzi wa katikati, huku David Silva na Andres Iniesta wakiwapa mipira Torres au Fabregas katika safu ya mashambulizi.

Vicente del Bosque akosolewa kuhusu mbinu yake
Vicente del Bosque akosolewa kuhusu mbinu yakePicha: Reuters

Kwa upande wa Prandelli, huenda akaanza na washambuliaji wawili, Antonio Cassano na shujaa wa magoli mawili katika nusu fainali, Mario Balotelli. Safu ya kati, Claudio Marchiso, Andrea Pirlo, Antonio Nocerino na Riccardo Montolivo, wanafaa kupewa fursa, na katika ulinzi, Giorgio Chiellini, Leonardo Bonucci na Frederico Balzaretti huenda wataanza. Iganzio Abata ambaye alikuwa akiuguza jeraha na kukosa mchuano wa nusu fainali dhidi ya Ujerumani huenda akarejea kikosini kwa fainali na kumrejesha benchi Andrea Barzagli.

Kipa Gianluigi Buffon atawaongoza Azurri kama nahodha katika fainali ya kesho na itakuwa mara ya kwanza kwa makipa wawili kuongoza timu zao kama manahodha katika fainali ya UEFA EURO. Mchuano huo utakuwa mgumu kiasi kamba hata mchambuzi wetu wa soka Ramadhani Ali ameshindwa kufanya uamuzi. Na wakati dimba la UEFA EURO 2012 likifikia kikomo kesho mjini Kiev, ufanisi wa kinyang'anyiro hicho haupimwi tu kwa kuzingatia nani atakayevikwa taji.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters/DPA/AFP
Mhariri: Miraji Othman