1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhispania yaiwacha Tahiti hoi

21 Juni 2013

Uhispania wamewapa Tahiti kichapo kikubwa cha mabao kumi kwa sifuri katika mechi ya kombe la mabara – Confederations Cup. Kwa mabingwa hao watetezi wa dunia na Ulaya, swali la pekee lilikuwa ni: magoli mangapi?

https://p.dw.com/p/18tlc
RIO DE JANEIRO, BRAZIL - JUNE 20: Fernando Torres of Spain goes past Mickael Roche of Tahiti on his way to scoring his team's third goal during the FIFA Confederations Cup Brazil 2013 Group B match between Spain and Tahiti at the Maracana Stadium on June 20, 2013 in Rio de Janeiro, Brazil. (Photo by Alexandre Loureiro/Getty Images)
Confed Cup 2013 Spanien TahitiPicha: Getty Images

Uhispania inayopigiwa upatu ilianza na wachezaji wa akiba dhidi ya Tahiti, katika mechi hiyo ya jana. Bahati mbaya kwa wapinzani wao, wachezaji wa “akiba” wa Uhispania waliwajumuisha washambuliaji watatu Fernando Torres, Juan Mata na David Villa, pamoja na viungo David Silva, Santi Carzola na Javi Martinez.

Tamasha za kabla ya mechi hiyo iliyochezwa katika uwanja wa Estadio Maracana mjini Rio de Janeiro zilikuwa ni pamoja na kikosi kizima cha Tahiti kuwapa mikufu wachezaji wote wa kikosi cha Uhispania.

Fernando Torres na DavId Villa walikuwa moto wa kutoea mbali katika safu ya mashambulizi
Fernando Torres na DavId Villa walikuwa moto wa kutoea mbali katika safu ya mashambuliziPicha: Getty Images

Ishara hiyo nzuri, hata hivyo, haikuizuia Uhispania dhidi ya kuizidi nguvu safu ya ulinzi ya Tahiti na kusukuma wavuni magoli kumi, huku Torres akifunga mabao manne, naye David Villa akitikisa mara tatu. Juan Mata alifunga goli moja naye David Silva akaweka mawili. Torres hata hivyo alikosa kufunga mkwaju wa penalti wakati zikisalia dakika kumi na tano mchuano kukamilika.

Mshambuliaji huyo wa Chelsea ambaye pia alifunga magoli matatu katika mechi moja kwenye mechi za kombe la mabara mwaka wa 2009, amesema ni ndoto kufunga magoli manne katika uwanja wa kama Maracana.

Nigeria wazidiwa nguvu na Uruguay

Katika mchuano wa pili, Diego Forlan alisheherekea mchuwano wake wa 100 akiichezea Uruguay kwa njia ya pekee, baada ya kusaidia kufungwa goli moja na kisha akafunga bao lake katika ushindi wao wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Nigeria, na kuisongeza timu yake karibu na awamu ya nusu fainali.

Ushindi wa Uruguay sasa umeliweka wazi kundi B
Ushindi wa Uruguay sasa umeliweka wazi kundi BPicha: Reuters

Beki wa Malaga, Diego Lugano aliiweka Uruguay kifua mbele kabla ya kiungi wa Chelsea John Obi Mikel kuisawazishia Nigeria. Uruguay na Nigeria zina pointi tatu kila mmoja katika kundi B lakini Uruguay itatarajiwa kushinda mechi ijayo dhidi ya Tahiti wakati Nigeria wakipambana na mabingwa watetezi wa kombe la dunia Uhispania.

Uhispania wanaongoza kundi hilo na pointi sita wakati Tahiti wakishikilia mkia bila pointi yoyote. Awamu ya mwisho ya mechi za makundi ni siku ya Jumapili.

Wakati huo huo, kiungo nyota wa Italia Andrea Pirlo atakosa mchuano wa mwisho wa makundi dhidi ya Brazil kutokana na jeraha la msuli wa mguu. Jeraha hilo limemwongezea matatizo ya viungo kocha Cesare Prandelli, kwa sababu kuna pengo la Danielle De Ross, ambaye atakosa mechi hiyo kwa sababu ya kadi mbili za njano. Italia waliwazidi nguvu Japan kwa mabao manne kwa mattau na wanatoshana na Brazil kileleni mwa kundi A kabla ya mechi ya Jumamosi ambayo itaamua mshindi.

Mwandishi: Bruce Amani/DW/AFP

Mhariri: Josephat Charo