1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhasama kati ya Schalke na Dortmund

22 Oktoba 2012

Ghasia zilizozuka baina ya mashabiki wa Borussia Dortmund na Schalke 04 katika mchuano wa 141 wa uhasimu wa eneo la Ruhr, ndizo zilizokuwa mbaya zaidi kuwahi kushudiwa katika miaka mingi.

https://p.dw.com/p/16UdO
Fußball Bundesliga 31. Spieltag: FC Schalke 04 - Borussia Dortmund am Samstag (14.04.2012) in der VeltinsArena in Gelsenkirchen. Die Polizei trennt die Dortmunder von den Schalker Fans in der Fankurve des Stadions. Foto: Friso Gentsch dpa/lnw
Fußball Derby Fans Borussia Dortmund FC Schalke 04Picha: picture-alliance/dpa

Watu 200 walikamatwa na wengine 11 kujeruhiwa katika purukushani hizo.Schalke ilipata ushindi wa magoli mawili kwa moja dhidi ya majirani wao Dortmund lakini ushindi huo uligubikwa na makabiliano kati ya mashabiki na polisi waliotumia mabomu ya kutoa machozi kutuliza rabsha.

Mgahawa mmoja uliharibiwa wakati mashabiki wakirusha mawe na kuutumia kama kinga. Miongoni mwa waliojeruhiwa ni polisi wanane, huku mashabiki 180, ikiwa ni 163 wa Schalke na 17 wa Dortmund wakikamatwa.

Dortmund walibaki kujishika viuno uwanjani baada ya mechi
Dortmund walibaki kujishika viuno uwanjani baada ya mechiPicha: picture-alliance/dpa

Katika matokeo mengine Borussia Bayer Leverkusen ilitoka sare ya kufungana magoli mawili kwa mawili na Mainz. Wolfsburg ikafungwa mawili bila jawabu na Freiburg. Eintracht Frankfurt iko katika nafasi ya pili ya ligi baada ya kuifunga Hanover magoli matatu kwa moja. Nayo Werder Bremen ikitikisa wavu mara nne kwa sifuri dhidi ya Bor. Moenchengladbach. Nuremberg ilitpoka sare ya bila kufungana na Augsburg, SV Hamburg ikafungwa goli moja kwa bila na Stuttgart. Felix Magath ni mkufunzi wa Wolfsburg ambayo kwa sasa inashikilia mkia. Bayern iliizaba Fortuna Düsseldorf magoli matano kwa sifuri siku ya Jumamosi.

Ligi ya Mabingwa

Mechi za ligi ya mabingwa barani Ulaya yaani UEFA Champions League zinarejea kesho Jumanne huku mabingwa watetezi Chelsea wakipambana na wapinzani kutoka Ukraine Shakhtar Donesk kwa mara ya kwanza katika duru ya tatu ya mechi za makundi.

Kwingineko katika kundi E, nchini Denmark Nordsjaelland inaikaribisha mabingwa wa Seire A Juventus huku timu zote mbili zikienga kupata ushindi wao wa kwanza katika dimba hili. Manchester United imeanza vyema katika kundi H wakati ikijaribu kuyaondoa mapepo yaliyoiabisha msimu uliopita walipoondolewa mapema. Baada ya kutoka nyuma na kushinda Stoke magoli manne kwa mawili mwishoni mwa wiki, sasa watapambana na Braga kutoka Ureno. Braga walishinda ugenini dhidi ya Galatasaray na kuendeleza rekodi yao ya kutoshinda ugenini barani Ulaya hadi mechi saba. Galatasaray nao watalenga kutafuta pointi zao za kwanza watakapocheza dhidi ya Cluj ya Romania. Celtic wana kibarua kigumu ugenini Catalonia kwa mchuano wa kundi G dhidi ya Barcelona. Vijana wa Neil Lennon waliwashinda Spartak Moscow magoli matatu kwa mwili mwanzoni mwa mwezi huu.

Frank Ribery ni mmoja wa wachezaji watakaoshambulia sana
Frank Ribery ni mmoja wa wachezaji watakaoshambulia sanaPicha: picture-alliance/dpa

Spartak and Benfica zitakabana koo katika mji mkuu wa Urusi katika mchuano mwingine wa kundi hilo. Wakati huo huo viongozi wa kundi E BATE Borisov watawakaribisha Valencia Belarus. Borisov wana pointi sita kutokana na mechi mbili baada ya kuwadiwaza Bayern Munich katika mechi iliyopita, lakini rekodi yao dhidi ya wapinzani wao wa Uhispania Valencia ni mbovu, kwa sababu hawajawahi kupata ushindi dhidi ya timu hiyo katika mechi sita za mwisho.

Lille watakabiliana na Bayern Munich katika uga wa nyumbani wa Grand Stade Lille Metropole. Borussia Dortmund itacheza dhidi ya Real Madrid katika wakati ambapo beki wake raia wa Poland Lukasz Piszczek amerefusha mkataba wake na mabingwa hao wa Ujerumani.

Borussia Dortmund watapambana na Real Madrid wa Uhispania
Borussia Dortmund watapambana na Real Madrid wa UhispaniaPicha: Reuters

Wakati huo huo, manahodha wa timu watakaocheza katika mechi za Champions League na Europa League wiki hii wataombwa kuvalia mkononi vitambaa vya kupinga ubaguzi wa rangi, kama sehemu ya kampeni ya kupambana na ubaguzi.

Shirikisho la soka Ulaya UEFA limesema linaunga mkono kampeni ya kundi la FARE, ambalo linalenga kuondoa ubaguzi wa rangi katika soka, kwa kuwataka manahodha wavae vitambaa mkononi vyenye maandishi 2“Unite against Racism“ yaani ungana dhidi ya ubaguzi.

Armstrong apokonywa mataji

Na mwendeshaji baiskeli Lance Armstrong amevuliwa mataji yake yote saba ya Tour de France na kupigwa marufuku ya maisha na Chama cha Kimataifa cha kuendesha baiskeli ICU. Chama hicho cha ICU kilisema kimetekeleza uamuzi uliochukuliwa mapema mwezi huu na Kitengo cha kupambana na matumizi ya dawa za kusisimua misuli nchini Marekani USADA. Rais wa chama cha ICU Pat McQuaid amesema Lance Armstrong hana tena nafasi katika uendeshaji baiskeli. Hii ni baada ya ripoti ya USADA kusema kwamba Armstrong alitumia mpango wa kisasa zaidi na wa kufana ambao hauchawahi kushuhudiwa katika mchezo huo.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman