1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ugiriki yatakiwa kuidhinisha mpango wa kubana matumizi

21 Juni 2011

Baada ya majadiliano ya miezi kadha umoja wa Ulaya hatimaye umekubaliana juu ya mfumo mpya wa kuyaokoa mataifa yenye madeni katika eneo la umoja wa sarafu ya euro.

https://p.dw.com/p/11frr
Waziri wa fedha wa Luxembourg Jean-Claude Juncker, ambaye ni mkuu wa mawaziri wa fedha wa mataifa ya eneo la euro.Picha: AP

Baada ya miezi kadha ya mjadala, umoja wa Ulaya umekubaliana kuhusu mfumo mpya na utakaodumu wa uokozi kwa mataifa wanachama yenye matatizo ya madeni katika eneo linalotumia sarafu ya euro. Waziri mkuu wa Luxemburg Jean-Claude Juncker , ambaye anaongoza kundi la mataifa wanachama wa sarafu ya euro, amesema mjini Luxemburg kuwa zaidi ya euro bilioni 500 zitatengwa kwa ajili ya mataifa yenye matatizo kuanzia mwaka 2013 na kuendelea. Hapo mapema, mawaziri wa fedha wa mataifa yanayotumia sarafu ya euro walichelewesha malipo ya mpango wa uokozi kwa Ugiriki, wakisema kuwa nchi hiyo ni lazima kwanza iweke hatua kali za kubana matumizi kabla ya kupokea fungu la tano la msaada wa dharura wenye thamani ya euro bilioni 12. Hata hivyo , shirika la fedha la kimataifa IMF, limeonya kuwa kushindwa kwa Ugiriki kuchukua hatua muhimu , kunaweza kusambaa kwa hali ya wasi wasi hadi ndani kabisa mwa eneo la euro na kusababisha kusambaa katika mataifa mengine duniani.