1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchumi wa Ujerumani umekabwa, lakini kuna tamaa baadae

23 Aprili 2009

Uchumi wa dunia unanywea, lakini wa Ujerumani zaidi

https://p.dw.com/p/Hcn9
Alama ya nembo ya Shirika la Fedha la Kimataifa, IMF.Picha: DW

Shirika la Fedha la kimataifa, IMF, katika makisio yake kuhusu hali ya baadae ya uchumi duniani na ambayo yalichapishwa punde hivi mjini Washington limechora rangi nyeusi ya mzozo ulivyo. Limetaja kwamba katika mwaka huu, uchumi wa Ujerumani utanywea kwa asilimia 5.6, hivyo kupungua zaidi waziwazi, ukilinganisha na uchumi wa nchi nyingine za viwanda. Na japokuwa katika nchi nyingi kubwa za viwanda, inatarajiwa uchumi utapanda hapo mwakani, lakini uchumi wa Ujerumani utakwenda chini kwa moja asilimia .

Kwanza kabisa, uchumi wa dunia unakwenda chini. Baada ya uchumi huo kukwama kabisa katika majira ya mapukutiko ya mwaka uliopita, uchumi wa dunia mwaka huu utapungua kwa 1.3 asilimia. Huo ndio wastani unaokisiwa kutokana na hali za harakati za kiuchumi katika nchi za viwanda na nyingi zinazoendelea. Sababu ya hali hiyo ni kwamba uchumi katika nchi kama vile Uchina na India utapanda. Nchi hizo zimepambana kwa nguvu uchuimi wao kwenda chini, lakini, licha ya mzozo ulioko duniani, zimeweza kupata nyongeza katika shughuli zao za kiuchumi, tena kwa kima ambacho nchi za kiviwanda katika nyakati nzuri zinaweza tu kukiotea.

Lakini ukweli ni kwamba hali ya uchumi wa dunia ni mbaya zaidi kuliko vile ule wastani unaozungumziwa. Hii inatokana na hali ya sasa ya kunywea uchumi huo na pia kunywea kunakotarajiwa, jambo ambalo Shirika la Fedha la Kimataifa, IMF, linakisia kutokea. Katika mwaka ujao wa 2010, IMF inataraji uchumi wa dunia utapanda chini kidogo ya mbili asilimia. Hicho sio kima kikubwa, lakini kutokana na zahama zilizotokea, bado ni kima kinachokubalika.

Hasa katika nchi za viwanda, hasa zile zilizokabwa na uchumi wao kwenda chini, kutakuweko na mkwamo wa harakati za kiuchumi. Ujerumani ni miongoni mwa nchi za viwanda ambazo hasa uchumi wao umekabwa vibaya. Hapa, hasara katika uchumi ni kubwa zaidi, na uchumi utabakia kuwa chini kwa muda mrefu zaidi. Wakati katika nchi za viwanda uchumi, kwa jumla, utanywea kwa asilimia 3.8, uzalishaji wa bidhaa hapa Ujerumani utakwenda chini kwa 5.6 asilimia. Huko ni kwenda chini sana kwa uchumi. Zaidi ni kwamba katika mwaka ujao, kwa mujibu wa makisio ya Shirika la IMF, ni kwamba uchumi wa Ujerumani, kinyume na uchumi wa nchi nyingi nyingine, hautapanda, bali utapungua kwa moja asilimia.

Hali hii isiokuwa ya kawaida kwa Ujerumani inatokana na sababu mbili: kwanza ni kutokana na Ujerumani uchumi wake kutegemea sana kuuza bidhaa zake nchi za nje, na sababu nyingine inatokana na watu ndani nchini hapa Ujerumani kupunguza kununua bidhaa. Katika wakati uchumi wa dunia unaponawiri, hapo Ujerumani inafaidika, na uchumi wa dunia unapokwenda chini, basi nayo Ujerumani inaumia. Karibu ya 45 asilimia ya bidhaa zinazotengenezwa Ujerumani zinakusudiwa kusafirishwa ngambo. Pale uchumi wa dunia unapokuwa mzuri, basi magari, mashine, viwanda, mazao ya kemikali, madawa, vyakula na miundo mbinu kamili, bidhaa za anasa na bidhaa nyingi nyingine kutoka Ujerumani hutakiwa katika nchi za nje. Sio tu nchi za viwanda zilizoendelea zinaagizia vitu hivyo vya Kijerumani, bali hata zile nchi zinazoinukia. Na pale mahitaji hayo yanapopungua duniani, basi Ujerumani huathirika sana. Kuna viwanda hapa Ujerumani ambavyo bidhaa zao zote ni kwa ajili ya kusafirishwa nje. Kuna viwanda vya aina hiyo ambavyo katika miezi iliopita vimepoteza 90 asilimia ya biashara zao.

Tena kuna suala kwamba watu wengi hapa Ujerumani wamepungukiwa na fedha kuweza kutumia katika kununulia vitu hapa nchini kuweza kuziba lile pengo linaloachwa kwa kushindwa kusafirishwa bidhaa za Kijerumani nchi za nje.

Lakini, jambo moja ni wazi, uchumi utapanda baadae, na Ujerumani itarejea tena kuchangia kw a ukubwa zaidi katika uchumi wa dunia. Shirika la Fedha la Kimataifa, IMF, katika makisio yake, linaona dalili ya mwanga mwisho mwa handaki. Na ushindani mkubwa wa kimataifa katika biashara lazima uambatane na watu wengi kuwa na uwezo kununua bidhaa hapa ndani nchini. Ni kwa njia hiyo tu ndipo Ujerumani, kwa njia ilio bora zaidi, itaweza katika siku za mbele, kukabiliana na hali ya uchumi wake kwenda chini.

Mwandishi: Karl Zawadzky/Othman/ZR

Mhariri: Josephat Charo