1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchambuzi wa magazeti ya Ujerumani

P.Martin25 Oktoba 2006

Mada inayochukua sehemu kubwa ya majadiliano ya kisiasa nchini Ujerumani ni mpango wa kutaka kubinafsisha huduma za ulinzi wa misafara ya ndege.

https://p.dw.com/p/CHUc

Wahariri wa magazeti ya Kijerumani leo hii wanaeleza maoni yao juu ya uamuzi wa Rais wa Ujerumani Horst Köhler kutotia saini amri ya kubinafsisha kwa sehemu,huduma za kulinda anga inayotumiwa kwa misafara ya ndege.Aliechambua magazeti ya leo ni Herbert Pechmann.

Tukianzia mji mkuu Berlin,gazeti la TAGESZEITUNG linasema:

“Hiyo jana,ile hatua ya iliyokubaliwa na Bunge kuruhusu ubinafsishaji wa huduma za kulinda misafara ya ndege,imezuiliwa na rais Horst Köhler kwa sababu hatua hiyo haimbatani na Katiba.Kwa hivyo,Köhler ameashiria kuwa suala la wajibu wa dola linakutikana katika Katiba ya nchi.Ni uzuri kuwa aliingilia kati,Katiba ilipopuuzwa na bunge kama vile kuhusu ulinzi wa misafara ya ndege.”

Kwa upande mwingine gazeti la STUTTGARTER ZEITUNG likitupia jicho uwezekano wa kuibadilisha katiba linaeleza hivi:

“Uwingi wa theluthi mbili bungeni unaweza kuamua kuwa usalama wa anga katika siku zijazo hautokuwa tena sehemu muhimu ya kile kinachoelezwa hivi sasa kuwa ni “jukumu la kisheria”.Rais wa Ujerumani tayari ameashiria kuwa hapo tena hatokuwa na upinzani:na tayari kuna dalili kwamba wanasiasa wanaelekea njia hiyo.Lakini suluhisho hilo haliambatani na taifa linalojichukulia kuwa makini.Ile ajali ya ndege iliyotokea Überlingen mwaka 2002 ni aina ya onyo.”

Gazeti la KIELER NACHRICHTEN nalo linachambua vipi wanasiasa wameathirika na uamuzi wa rais.Kwa maoni ya mhariri wa gazeti hilo,”Hatua ya rais kukataa kutia saini,imewawatahayarisha wanasheria.Kwani kukataa kwa sababu zinazohusika na sheria si jingine isipokuwa kwamba sheria hiyo ina uzembe.Köhler lakini anaeleza kuwa anaelewana na hatua ya kuibadilisha katiba.Lakini rais ni mtu wa mwisho wa kuhimiza mageuzi ya katiba lamalizia Kieler Nachrichten.

Kwa upande mwingine mhariri wa ALLGEMEINE ZEITUNG kutoka Mainz,anatupia jicho upande unaohusika na fedha.Anasema:

“Euro bilioni moja ni pesa nyingi sana.Huenda ikawa serikali ilijikwaa kikatiba kwa sababu ya kitita hicho cha pesa na kutaka kuuza sehemu kubwa ya huduma za usalama za Ujerumani.Kwa hivyo kukataliwa kutiwa saini na rais ni pigo kali kwa wanasiasa.Viongozi hao wamefanya kosa na wameadhibiwa.Na hilo ni barabara.”Hayo ni maoni ya ALLGEMEINE ZEITUNG.