1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uamuzi wa serikali ya muungano kuhusu nishati ya nuklea wakosolewa magazetini

Oumilkher Hamidou7 Septemba 2010

Watakaofaidika na uamuzi wa kurefusha muda wa vinu vya nishati ya kinuklea ni wenye kumiliki makampuni makubwa makubwa ya nishati-wanasema wahariri

https://p.dw.com/p/P5wp
Wapinzani wa nishati ya nuklea waporomosha piramidi ya mapiga (bandia)ya takataka za kinuklea karibu na lango la Brandenburger Tor mjini BerlinPicha: AP

Kurefushwa muda wa matumizi ya nishati ya kinuklea na hukmu ya korti ya mjini Munich dhidi ya vijana 2 waliompiga hadi kufa Dominik Brunner ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa zaidi na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.

Tuanze lakini na uamuzi wa serikali kuu ya muungano wa nyeusi na manjano wa kurefusha muda wa vinu vya nishati ya kinuklea.Gazeti la "Fuldaer Zeitung" linaandika:

"Kama uamuzi wa serikali kuu ambao kansela anausifu kuwa ni wa "kimapinduzi" na waziri wa mambo ya nchi za nje kuutaja kuwa ni "wa enzi",utatekelezeka kweli,hakuna ajuaye.Kwanza yaonyesha kana kwamba kisa hicho kitaangukia katika korti kuu ya katiba kwasababu serikali kuu haijazishirikisha serikali za majimbo katika kupitisha uamuzi huo.Na baadae,mnamo miaka ijayo masuala yote ya ziada kuhusu uamuzi huo yatachomoza,mfano wa vimondo angani,baada ya upande wa upinzani kutangaza kwamba watabatilisha uamuzi huo pindi wakiingia madarakani.Hali hiyo haiyarahisishii mambo makampuni ya nishati."

Gazeti la "Landeszeitung" linaandika:

Kansela anazungumzia juu ya mapinduzi.Na hajakosea.Hasa pale anapomaanisha mapinduzi ya kuachana na mpango wa kuachana na nishati ya kinuklea.Au mapinduzi katika masoko ya hisa.Kwasababu faharasa za makampuni ya nishati zimepanda kupita kiasi.Si ajabu,wao ndio wanaofaidika na kile kiitwacho mswaada wa nishati.Ikiwa tarakimu za taasisi za wanaopigania usafi wa mazingira zinaaminika basi makampuni ya EON na mengineyo yatajikingia faida ya zaidi ya Euro bilioni mia moja.Badala ya kuleta mageuzi katika sekta ya nishati,kansela anarejea nyuma.Anaamua bila ya kuzingatia maoni ya wananchi walio wengi.Anawapa nguvu wenye kumiliki makampuni ya nishati badala ya kuwadhoofisha.Na kwa namna hiyo anachochea mapinduzi mengine:mashirika,vyama vya upinzani,vyama vya wafanyakazi na wapinzani wengine wote wa nishati ya kinuklea watamjibu kupitia maandamano majiani.

Superteaser NO FLASH Deutschland Prozeß Gericht Urteil Brunner-Prozess München
Domonik Brunner ameangukia mhanga wa matumizi ya nguvu ya vijana Markus S na Sebastian LPicha: picture alliance/dpa

Mada yetu ya pili magazetini inahusu hukumu iliyopitishwa na korti ya mjini Munich dhidi ya vijana wawili waliompiga hadi kufa bwana mmoja aliyekuwa akiwahami watoto wadogo.Gazeti la "Westdeutsche Zeitung" la mjini Düsseldorf linaandika:

Mtu anaweza kusema hukmu hiyo "ni kali,lakini imestahili"-mambo yakesha.Lakini hayo yasingetosha kuhalalisha uamuzi wa hakimu wa mjini Munich.Kwa kupitisha hukmu hiyo,korti ya mji huo imetaka kuleta mkondo mpya katika hukmu dhidi ya visa vya matumizi ya nguvu vinavyofanywa na vijana.Kiini hapo ni kwamba kumkanyaga mtu kichwani,´na juu ya tumbo wakati mtu huyo ameshaanguka ni sawa na kudhamiria kuuwa.Kwa namna hiyo hukmu ya korti ya mjini Munich ni onyo bayana kwa vijana wenye kutumia maguvu,mahakama itachukua hatua kali zinazostahiki dhidi yao.

Gazeti la Münchner Merkur linaandika:

Markus S. na Sebastian L. wanabeba jukumu la kifo cha meneja Brunner.Kwa hivyo lazma waadhibiwe.Hata kama katika sheria zinazohusu makosa ya jinai kwa vijana -haijatajwa kua ni adhabu.Inatajwa kua ni ulezi.Ulezi ambao ungebidi uanze mapema zaidi:nyumbani,katika shule za chekechea na shuleni.Katika kaadhia ya Dominik Brunner imebainika sio tuu wazee wa washtakiwa walioshindwa kuwajibika ipasavyo,bali pia waalimu, wasimamizi wa huduma za jamii na idara husika walishindwa kuwarudi vijana hao.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir (Inlandspresse)

Mpitiaji:Abdul-Rahman