1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump kuamua kuhusu mkataba wa Paris

Sekione Kitojo
1 Juni 2017

Wahariri wa magazeti hapa Ujerumani wamejishughulisha zaidi na mada inayohusu uamuzi unaotarajiwa na rais Donald Trump katika  kujitoa ama kubakia katika mkataba wa kimataifa wa Paris wa mabadiliko ya tabia nchi,

https://p.dw.com/p/2dyH1
USA Donald und Melania Trump Abreise aus Tel Aviv
Rais wa marekani Donald Trump Picha: Getty Images/AFP/M. Ngan

Wahariri  pia  wamejishughulisha  na  hali  nchini  Afghanistan  baada  ya  shambulio  la  kigaidi ambapo  watu  zaidi  ya  80  waliuwawa  jana.

 

Dunia imelazimika  kusubiri kwa   siku  chache  kuweza  kufahamu msimamo  wa   rais  wa  Marekani  Donald  Trump,  kuhusiana  na iwapo  atakubali  kuwamo ndani  ya   mkataba  huo  wa  kimataifa ama  ataamua   vingine. Lakini  baada  ya kuhudhuria  mikutano  ya viongozi  wa  jumuiya ya kujihami ya NATO  mjini  Brussels  na  ule wa  nchi  zenye  utajiri  mkubwa wa  viwanda  G7  mjini  Taormina, Italia, huenda  matumaini  yakawa  yamepotea, na  kwamba  ni maajabu  tu yanaweza  kutokea  ili  kuweza  kumfanya  rais  huyo wa  Marekani  kuweza  kuliangalia  suala  la  mabadiliko  ya  tabia nchi  katika  uhalisia  wake. Itakuwa  hatari  sana  kwa  Marekani kujitoa  kutoka  mkataba  huo, kwa  kuwa  huo  ndio  utakuwa mwisho  wa  ulinzi wa  mazingira  kimataifa. Vizingiti  vingi  mno vimeondolewa, tangu  mkutano  wa  Paris, lakini kila  mara kunatokea kitu kingine kinakinga.

 

Gazeti  la  Hannoversche Allgemeine Zeitung  likiandika  kuhusu mada  hiyo  ya  mkataba  wa  mazingira, mhariri  anaandika, kwamba kujitoa  kwa Trump  kutoka  mkataba  wa  mazingira  ni  ahadi aliyoitoa  wakati  wa  kampeni  ya  uchaguzi nchini  Marekani. Mhariri anaendelea.

 

Katika eneo  la  kati  nchini  Marekani  wananchi  wanashangiria akifanya  hivyo. Mara chache  kauli  ya "mimi sijali"  inakuwa  na maana nzuri.  Kile  anachoonesha  rais  huyu  wa  45  wa  Marekani Donald Trump kuhusu  suala  hili  la  mazingira ni  kwamba  anajaribu kwa  njia  ngumu  sana  kujaribu  kuleta  kitu  cha  manufaa. Kwa upande  wa  kisiasa  hadi  sasa  hajaleta  chochote  cha  kujivunia. Lakini  ana   madaraka  kuweza  kuvuruga  mambo. Mojawapo  ya mambo  hayo  ni  kuvuruga  msingi  wa  mabadiliko  ya  mfumo  wa afya  ambao  umewekwa  na  mtangulizi  wake Barack Obama, ameshambulia  kwa  ndege  za  kivita  nchini  Syria  na  sasa anataka  kuondoa  yale  yote  yaliyopatikana  kwa  miaka  mingi  ya majadiliano  katika  mkataba  wa  mazingira  wa  Paris.

Shambulizi la kigaidi Afghanistan

Mada  nyingine  ni  kuhusu  shambulio la bomu  lililotokea  nchini Afghanistan  jana ambapo watu  zaidi  ya  80  waliuwawa. Mhariri wa  gazeti  la  Reutlinger General-Anzeiger  anaandika  kwamba , kundi  la dola la kiislamu IS  huenda linataka  kuleta  mtafaruku miongoni  mwa  mataifa  ya  magharibi  katika kulishughulikia  suala hilo. Mhariri  anaendelea  kuandika.

Afghanistan Kabul nach Anschlag
Uharibifu baada ya shambulio la bomu mjini Kabul AfghanistanPicha: picture-alliance/dpa/Hedayatullah Amid

Kundi  la  Taliban  limeonesha  hivi  karibuni  kutaka  kuzungumza  na serikali  mjini  Kabul  huenda  ni  kutokana  na  kutambua  mbinyo  wa ushindani  kutoka  makundi  mengine  ya  wapiganaji  ndani  ya  nchi hiyo  hususan kundi  la  IS. Rais  wa  Afghanistan  Ashraf Ghani  kwa hilo  yuko  tayari. Ushahidi ni  mfano  wa  Gulbudidin Hekmatyar. Imewezekana  kufanya  makubaliano  ya  amani  na  mbabe  huyu wa  zamani  wa  vita. Hekmatyar  sasa  sio  tena  Taliban,  lakini wito  wake  wa  kumaliza  vita,  una  uzito  mkubwa. Wanapaswa kukaribiana  kisiasa. Kupeleka  wanajeshi  zaidi  katika  jimbo  la Hindukush sio  suluhisho.

 

Mhariri  wa  gazeti  la  Nordwest - Zeitung  kutoka  Oldenburg anaandika  kuhusu  mada  hiyo kwamba  wakati  mataifa  ya magharibi  yalipoanza  kupunguza  majeshi  yao  nchini  Afghanistan vita  vilikuwa  bado  havijamalizika.  Mhariri  anaendelea.

 

Ni kama Carl von Clausewitz  alivyosema katika  karne  ya  19 kwamba, Iwapo hutaweza  kumshinda, kuna  hatari kwamba umeshindwa. Kwa hiyo kuna fursa  mbili tu, tuiache  Afghanistan ama  tuingilie  kati kwa  kiwango  kikubwa zaidi. Kufanya hivyo nusu nusu hakutasaidia.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / Inlandspresse

Mhariri: Josephat Charo