1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump aikosoa NATO

Shisia Wasilwa
10 Julai 2018

Rais Donald Trump wa Marekani amesema mataifa ya Ulaya ndiyo yanayofaidika zaidi na Jumuiya ya kujihami ya NATO kuliko Marekani, huku anapoelekea Brussels kwenye mkutano wa jumuiya ya Kujihami ya NATO siku ya Jumatano.

https://p.dw.com/p/319nD
Donald Trump und Melania fliegen nach Brüssel
Picha: picture-alliance/dpa/P. M. Monsivais

Akijibu tamko la rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya Donald Tusk aliyesema kuwa anapenda kulalamika kila siku, Trump alijitetea kwa kusema kuwa alikuwa anarejelea uwiano wa biashara na mchango wa Marekani kwa Jumuiya hiyo ya NATO. 

Akizungumza na wanahabari katika Ikulu ya White House kabla ya kuondoka Washington kuelekea kwenye  mkutano wa Brussels, rais Trump alisema Jumuiya ya NATO iliyodumu kwa miaka 69 inawafaa zaidi watu wa Ulaya kuliko Wamarekani.

Rais Trump amesema, "kwa sasa siwezi kusema iwapo rais wa Urusi Vladimir Putin ni rafiki au adui." Trump atahudhuria kikao cha Jumuiya ya Kujihami ya Nato ambapo atashiriki kwenye mazungumzo ya kibiashara kabla ya kufanya kikao kingine na rais Putin wa Urusi jijini Helsinki juma lijalo. Jens Stoltenberg ni katibu mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO, anasema kuwa historia imeonyesha sio mara moja kuwa tofauti kati ya mataifa wanachama yanapoibuka Jumuiya hiyo imeweza kupata ufumbuzi. "Ni kwa maslahi yetu kuidumisha NATO. Ni jambo jema kwa Ulaya, lakini pia ni jambo zuri kwa Marekani Kaskazini. Hapa Ulaya tuna vikosi vyetu vya wanajeshi, miundo mbinu ya ulaya ambayo si tu muhimu kwetu kwa ulinzi wa Ulayalakini kwa jeshi la Marekani kutumia kwa shughuli zake Mashariki ya Kati na barani Afrika. "

Belgien EU NATO Donald Tusk, Jens Stoltenberg und Jean-Claude Juncker
Kushoto Donald Tusk wa Baraza la Umoja wa Ulaya, katikati Jens Stoltenberg wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO na kulia ni Jean-Claude Junker Picha: picture-alliance/AP Photo/G. V. Wijngaert

Trump: Marekani inanyanyaswa

Trump anatarajia kuwa na mazungumzo magumu na Jumuiya hiyo ya Kujihami ya NATO kuhusu fedha za kutumiwa katika masuala ya ulinzi. Ameongeza kusema, "ushirika na Urusi, China na mataifa mengine ni jambo zuri wala sio baya."

Kwa muda mrefu Trump amekuwa akiwakosoa washirika wa Marekani kuhusu Jumuiya ya NATO, akiyashinikiza mataifa wanachama kutimiza ahadi zao za kutenga asilimia mbili ya jumla ya mapato ya mataifa yao kwa ulinzi ifikapo mwaka 2024.

Kwenye mtandao wa kijamii wa twitter Trump aliandika kuwa Marekani inatumia fedha nyingi zaidi kuyalinda mataifa hayo. Hiyo si haki kwa mlipa kodi na kuongeza kusema, maandishi ambayo huenda yakaibua mvutano  kwenye meza ya mazungumzo.

Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya Donald Tusk ameelezea tabia ya Trump kuwa "changamoto kwa Ulaya sawasawa na kupanuka na kukua kwa uchumi wa China ama uhasama wa Urusi."

Kwenye mkutano wa Mataifa ya Kujihami wa NATO, viongozi watajadili uhasama wa Urusi, lakini mtihani mkubwa utakuwa ni mazungumzo baina ya rais wa Urusi Vladimir Putin na Donald Trump.

Mwandishi: Shisia Wasiwa, Dpa, Ap

Mhariri: Yusuf Saumu