1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Timu sita zatinga robo fainali

27 Juni 2016

Ufaransa, Ujerumani na Ubelgiji zilijikatia tikiti zao za kucheza robo fainali wakati timu hizo tatu kati ya zile zinazopigiwa upatu kutwaa taji hilo zikitimiza ahadi yao

https://p.dw.com/p/1JEUG
UEFA EURO 2016 - Achtelfinale | Deutschland vs. Slowakei 1. Tor Boateng feiert
Picha: Reuters/C. Recine

Kulikuwa na hali ya tumbo joto miongoni mwa mashabiki wa Ufaransa wakati timu yao ilifungwa bao katika kipindi cha kwanza, lakini hali ikarejea ya kawaida katika kipindi cha pili wakati Les Bleus walishinda 2-1 dhidi ya Jamhuri ya Ireland.

Na wakati Ufaransa ililazimika kutoa jasho kabla ya kufuzu, Ujerumani haikuwa na changamoto za aina hiyo baada ya kuibamiza Slovakia 3-0. Joachim Löw ni kocha wa Ujerumani "kuna hisia nzuri wakati timu inapokuwa nzuri katika ulinzi. lakini sio kila mara suala la ulinzi, lakini pia mchezaji aliyeko mbele, Thomas Muller, Mario Gomez, Julian Draxler, Mesut Özil wote wako sawa. Tuliinyima Slovakia fursa ya kuwa mchezoni na hivyo safu yetu ya ulinzi ikawa na kazi rahisi. timu yote inawajibika katika kazi ya ulinzi.

UEFA EURO 2016 - Achtelfinale | Ungarn vs. Belgien | Torjubel Alderweireld
UPicha: Reuters/C. Platiau

Ubelgiji nayo ilionekana kuwa moto wa kuotea mbali baada ya kuimbumburusha Hungary 4-0 katika mchuano ambao Eden Hazard alikuwa moto wa kuotea mbali.

Lakini mabao na ubora wa kandanda katika mechi hizo tatu za jana, vilionyesha kuimarika kwa mchezo mbovu ulioshuhudiwa Jumamosi wakati Poland, Wales na Ureno ziliingia katika robo fainali. Ureno ilivunja nyoyo za Croatia kwa kufunga bao katika dakika za mwisho za kipindi cha ziada na kuipa Ureno ushindi wa moja bila. Ureno sasa wataumana na Poland katika robo fainali.

Poland iliipiku Uswisi 5-4 kupitia mikwaju ya penalty baada ya mpambano kukamilika kwa sare ya 1-1 katika dakika 120. Wales ilipata ushindi wa 1-0 baada ya Ireland ya Kaskazini kujifunga bao katika lango lao wenyewe. Wales sasa wataangushana na Ubelgiji katika robo fainali

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri: Yusuf Saumu