1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TEHRAN : Mkutano wa Maagamizi ya Wayahudi wafanyika Iran

11 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCkL

Iran leo imekaidi shutuma za jumuiya ya kimataifa kwa kufunguwa mkutano wenye lengo la kuvunja miiko juu ya Maanagamizi ya Wayahudi na kuhudhuriwa na wataalamu kadhaa wa historia wa mataifa ya magharibi wanaotaka kubadili ukweli wa mambo juu ya maangamizi hayo.

Iran inasema mkutano huo unakusudia kutowa uwanja kwa wanahistoria kutowa maoni yao huru juu ya Maangamizi hayo ya Wayahudi yaliofanyika wakati wa utawala wa Manazi wa Ujerumani lakini mataifa ya magharibi wanaupinga mkutano huo kwa kusema kwamba unataka kukana kuangamizwa kwa umma wa Wayahudi milioni sita katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Akifunguwa mkutano huo Rasoul Mousavi Mkuu wa Taasisi ya Siasa na Masomo ya Kimataifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ambayo ndio inayoandaa mkutano huo wa siku mbili amesema mkutano huo hautaki kukanusha wala kukubali kuwepo kwa Maangamizi ya Wayahudi bali ni kutowa nafasi ya mazingira muafaka ya kisayansi kwa wasomi kutowa maoni yao kwa uhuru juu ya suala hilo la kihistoria.

Zaidi ya watafiti 60 wa kigeni kutoka nchi 30 wanahudhuria mkutano huo.

Rais Mahmoud Ahmedinejad wa Iran huko nyuma ameyaita maangamizi hayo ya Mayahudi milioni 6 wakati wa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia kuwa ni uzushi.

Jumuiya ya Kimataifa imelaani vikali mkutano huo.