1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Stella Nyanzi aachiwa kwa dhamana

10 Mei 2017

Msomi huyo na mwanaharakati maarufu wa haki za wanawake na wasichana aliwekwa rumande kwa mwezi mmoja na kufunguliwa mashtaka ya kutumia mtandao vibaya. Alimkosoa Museveni na mkewe ambaye ni waziri wa elimu.

https://p.dw.com/p/2ckUs
Stella Nyanzi
Picha: Reuters/J. Akena

J3.10.05.2017. Stella Nyanzi released on bail - MP3-Stereo

Hata hivyo hakimu ametoa masharti kwa msomi huyo kuhakikisha kwamba yeye na wenzake hawasambazi taarifa zozote ambazo zinahusiana na kesi dhidi yake ya kutumia vibaya mitandao ya kijamii kumvunjia heshima rais Museveni na mke wake Janet pamoja na utawala kwa jumla.

Kufuatia mashaka kuwa Stella angekamatwa mara tu baada ya kuachiwa na mahakama, wafuasi wake walijiandaa kumpokea kutoka kwenye korokoro ya muda ili kuepusha fursa yoyote kwa waliotarajiwa kumkamata kufanya hivyo. Walimbeba hadi kwenye gari moja binafsi na likaondoka mahakamani kwa kasi kubwa kiasi kwamba jaribio la wanahabari kupata angalau kauli yake halikufua dafu.

Stella anakabiliwa na mashtaka ya kutumia vibaya mitandao ya kijamii kumvunjia heshima rais Museveni na mke wake Janet Kastaha katika harakati zake za kuitaka serikali itoe pedi za bure za hedhi kwa wasichana nchini. Rais Museveni alikuwa ameahidi kufanya hivyo katika kampeni zake mwaka jana lakini mkewe ambaye ni waziri wa elimu alitangaza baadaye kuwa hilo halingewezekana.