1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

STASI

3 Novemba 2009

Katika msururu wetu wa ripoti kuhusu miaka 20 tangu kuporomoka kwa ukuta wa Berlin na kuungana tena kwa nchi mbili za Ujerumani,leo tunaikodolea macho Idara ya Usalama ya iliokuwa Ujerumani Mashariki (STASI):

https://p.dw.com/p/KDcq
Kanzela Angela Merkel(Kushoto) alipotembelea makao makuu ya STASI.Picha: AP

Ukizungumzia (GDR)-Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani, jambo la kwanza linalokujia kichwani, ni Idara hiyo ya Usalama (STASI)-ufupisho wa "Wizara ya Usalama wa dola ".

"STASI" ilikuwa Idara ya upelelzi iliokuwa na askari kanzu wengi na zana nyingi za kuwachungua na kuwapeleleza wananchi wake wenyewe.Ilikuwa pia na tawi la kutisha ambalo jukumu lake kuu, ni kumfanyia ujasusi adui mkuu wa kinadharia na usoni kabisa ilikuwa Ujerumani Magharibi.Azma ilikua kuwapandikiza ndani yake majasusi kadhaa.Baadhi ya wakati hii ilifanikiwa na wakati mwengine haikufanikiwa sana.

Idara ya usalama ya Ujerumani Mashariki (STASI) kwa ufupi, daima ikigonga vichwa vya habari na hata miaka 20 baada ya kuvunjwa kabisa yaendelea kugonga vichwa vya habari.Katika visa vyake vilivyogonga mno vichwa vya habari ulimwenguni na nchini,ni kufichuliwa kwa jasusi wake mkubwa 1974, Günther Guillaumme, ambae alikuwa mjumbe -msaidizi binafsi wa Kansela Willy Brandt na kwa miaka kadhaa akipeleka habari Berlin ya Mashariki kutoka afisi ya Kansela Bonn .

Idara ya Usalama hiyo ilijiingiza pia miongoni mwa makundi ya wanafunzi na hata ndani ya Idara za usalama za maadui zake ilikuwa na wapelelezi wao.

Ripota huyo anasimulia:

"Barabara hii imegeuka kama medani ya vita.Kumezuka mapambano kadhaa kati ya Polisi na waandamanaji."

Tarehe 2,Juni,1967 maelfu ya watu waliandamana Berlin Magharibi kupinga ziara ya Shah wa Iran. Shahidi mmoja alisema:

"Ghafla, nilijionea bastola ikifyatuliwa .Halafu nikaona mhanga alivyoanguka chini nyuma ya motokaa na hatikisiki tena."

Kijana huyo, alijionea hapo mwanafunzi Benno Ohnesorg , akiaga dunia.Risasi hiyo ilifyatuliwa na polisi aitwae Karl-Heinz Kurras.Ni mwaka huu na kwa bahati nasibu tu katika kulitupia macho daftari moja iligunduliwa kuwa, risasi ile ilifyatuliwa kwa amri ya STASI-Idara ya Usalama ya Ujerumani Mashariki.Ni mkasa ambao ilikuwa taabu kuamini hata kwa mchunguzi wa kisa hicho Helmut Müller-Engberg.

Students march through downtown Munich, West Germany, June 5, 1967 carrying a banner reading "Benno Ohnesorg - political murder" to commemorate the fatal shooting of German student Benno Ohnesorg. Ohnessorg was fatally shot during an anti Shah protest in West Berlin, June 2, 1967 by police officer Karl-Heinz Kurras. (AP Photo/Helmuth Lohmann
Wanafunzi wakiandamana mjini Munich kumkumbuka Benno Ohnesorg aliyeuliwa na polisi Karl-Heinz KurrasPicha: AP

Tangu mwanzoni mwa miaka ya 1990,Müller-Engberg, akichunguza katika Idaraya usalama ya STASI mjini Berlin,ujasusi uliokuwa ukifanywa na Idara hiyo upande wa magharibi.Akagundua visa vingi vya kusisimua:

Müller anasema:

"Kwamba Polisi wa Berlin magharibi akiwa katika nafasi nzuri kazini,anapatiwa silaha na Idara ya STASI kwa kupewa fedha kununulia bastola chapa P 38 ni jambo la kusangaza." Amekumbusha Müller-Engberg.