1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Siwezi kumpigia goti Erdogan-Schulz

Saumu Mwasimba
16 Septemba 2017

Mgombea ukansela na mkuu wa chama cha SPD Ujerumani Martin Schulz azungumza na DW na kusema katu katu hawezi kumpigia magoti rais wa Uturuki akisema Ujerumani haipaswi kushinikizwa

https://p.dw.com/p/2k6T1
Deutschland wählt DW Interview mit Martin Schulz
Picha: DW/R. Oberhammer

Mgombea wa Ukansela wa chama cha Social Democratic SPD nchini Ujerumani Martin Schulz amezungumza na DW leo(16.09.2017) na kujieleza msimamo wake kuhusiana na masuala kadha ikiwemo pia mvutano na Uturuki pamoja na suala la mkataba wa wakimbizi uliofikiwa na Umoja wa Ulaya na Uturuki.Akihojiwa mjini Freiburg na mhariri mkuu wa DW  Ines Pohl pamoja na mtangazaji  Jaafar AbdulKarim -Schulz amesema ikilazimika  mkataba juu ya wakimbizi ufutiliwe mbali  Schulz amesisitiza kwamba Ujerumani haipaswi hata mara moja kujiweka chini mbele ya Uturuki.

''Siko tayari kumpigia magoti bwana Erdogan.Mtu hapaswi kuridhia kushinikizwa''

Ikiwa ni siku nane zimebakia kabla ya uchaguzi nchini Ujerumani mgombea huyo wa SPD amemkosoa kwa maneno makali rais wa Uturuki Erdogan akisema hali ya haki za binadamu nchini Uturuki imezidi kuwa mbaya.

''Kwa mwandishi habari yoyote atakayekwenda katika nchi hiyo kuripoti kwa hivi sasa siwezi  kumhakikishia kwamba hatoishia jela''

Kadhalika Schulz amesema kwa hali inayoendelea hivi sasa nchini Uturuki chini ya rais Recepp Tayyip Erdogan haoni sababu yoyote ya nchi hiyo kupewa fursa ya kujiunga na Umoja wa Ulaya na kwamba haina maana yoyote kuzungumza na rais huyo wa Uturuki kwa sasa.

Deutschland wählt DW Interview mit Martin Schulz
Picha: DW/R. Oberhammer

Ana mipango gani juu ya haki ya wahamiaji barani Ulaya

Schulz anataka kuwa muwazi akifanikiwa kuwa Kansela hata atakapozungumza na nchi za Umoja wa Ulaya ambazo zinakwepa kuwapokea wakimbizi akisema

''ushirikiano ni kitu cha msingi katika masuala ya kusimamia gharama lakini pia kugawana wakimbizi''

Pia ametowa mwito wa kuundwa sheria ya Uhamiaji itakayoweka kiwango maalum katika Umoja wa Ulaya lakini vile vile sheria hiyo isiguswe. Akijibu suali aliloulizwa ikiwa anaweza kushirikiana na nchi zinazoendeshwa na madikteta barani Afrika ili mradi afikie lengo la kuwazuia wakimbizi kuingia barani Ulaya. Schulz amesema inawezekana kushirikiana na nchi za kanda hiyo hata zile ambazo hazizingatii utawala wa kidemokrasia kukabiliana na wimbi la wakimbizi wanaokuja Ulaya,lakini pia  akasisitiza suala hili linawezekana tu kwa ushirikiano na usimamizi wa taasisi za Kimataifa.

Mwandishi:Saumu Mwasimba

Mhariri:Sudi Mnette