1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Siku ya Chakula Duniani

Maja Dreyer16 Oktoba 2007

Kila mwaka tarehe 16 ni siku ya chakula duniani ikiwa ni tarehe ya kuadhimisha kuasisiwa kwa shirika la chakula duniani FAO mnamo mwaka 1945. Mwaka huu maneno makuu ya siku hii ni “Haki ya kupata chakula”. Haki hiyo lakini haitekeleziwi kwa watu wasiopungua Millioni 850 ulimwenguni kote.

https://p.dw.com/p/C7rr
Alame nyekundu ni maeneo yaliyokumbwa zaidi na njaa
Alame nyekundu ni maeneo yaliyokumbwa zaidi na njaaPicha: FAO

“Kutokuwa na njaa ni nia ya msingi iliyowekwa katika katiba ya Shirika la FAO.” Anayesema haya ni Jacques Diouf, mkuu wa shirika hilo la chakula duniani, katika hotuba yake mbele ya siku ya chakula.

Aidha, Bw. Diouf anatoa mwito kwa mataifa yote duniani kutekeleza ahadi yaliyoitoa: “Kwenye mkutano wa kilele wa mwaka 1996, viongozi wa nchi na serikali walithibitisha haki ya kila mmoja kuweza kupata chakula safi kinacholisha vizuri pamoja na haki ya kila mtu kutokumbwa na njaa. Pia walijipa sharti kutekeleza haki hiyo hatua kwa hatua ili kuhakikisha upatikanaji wa chakula kwa wote.”

Tangu Jaqcues Diouf alipochaguliwa madarakani hapo mwaka 1994, mengi yalibadilika katika taratibu za shirika la FAO. Shughuli nyingi haziendeshwi tena na ofisi za makao makuu huko Roma, Italy, bali zinafanywa na ofisi katika nchi husika. Aidha ushirikiano na sekta ya uchumi na mashirika yasiyo ya kiserikali uliongezeka na vilevile shirika la FAO liliongeza idadi ya wataalamu kutoka nchi zinazoendelea.

Lakini hali ya chakula duniani haikubadilika. Bado njaa ni tatizo kubwa, na mataifa yaliyoko kusini mwa jangwa la Sahara barani Afrika yanakabiliwa mno na balaa hiyo. Nchi nyingi zinategemea msaada wa vyakula kutoka nje. Mkurugenzo wa FAO, Jacques Diouf, lakini anasisitiza kwamba chakula ni haki ya msingi na si kitu cha kuomba: “Haki ya chakula inatulazimika kubadilisha fikra zenu, kwani si sadaka bali ni haki. Kuhakikisha kuwa bila binadamu anapata chakula cha kutosha na kizuri siyo tu kufuatilia maadili mazuri au kuwekeza katika binadamu. Zaidi ni kutekeleza haki ya msingi ya kibinadamu, na dunia hii ina utajiri wa kutosha kuitekeleza.”

Kila taifa linabeba jukumu kuondosha njaa ya wananchi wake. Unakuta kuwa umaskini, yaani njaa, maradhi mengi, uhaba katika elimu na sekta ya afya – unatokea pale ambapo sekta ya kilimo haijarekebishwa kutokana na sera mbaya, mizozo au rushwa. Nchi mbili ambazo tangu hivi karibuni zimeendelea haraka kiuchumi, India na China, ziligeuka tu baada ya kurekebisha sekta yao ya kilimo. Kila tunachokiita “Mapinduzi ya kijani” ni msingi wa vita dhidi ya umaskini na njaa.

Hata hivyo, si juu ya nchi husika tu. Tangu miaka mingi iliyopita, Umoja wa Ulaya na Marekani iliharibu ukulima katika nchi zinazoendelea kuwa kulipa ruzuku kubwa kwa wakulima wao. Baada ya mkutano mkuu uliopita wa Umoja wa Mataifa, rais Bush wa Marekani aliarifu kwamba vyakula vinavyohitajika kwa msaada vinunuwe barani Afrika badala ya kwengineko.

Mratibu wa Umoja wa Mataifa kwa malengo ya millenia ambayo moja kati yao ni kupunguza umaskini na njaa duniani, Bi Eveline Herfkens, anadai nchi tajiri zisimamishe malipo yao ya ruzuku kwa wakulima na kufungua masoko yao kwa nchi zinazoendelea. Bi Herfkens alisema: “Theluthi mbili ya watu maskini wanaishi mashambani na wanategemea ukulima. Wakati sisi wa nchi za Ulaya tunapoendelea kuathiri maisha yao kwa kulipa ruzuku kwa wakulima wetu na kufunga masoko yetu makubwa, hatufikia malengo ya maendeleo. Kwa hivyo, si tu msaada ulio muhimu bali pia sera za biashara.”

Hadi sera zitakapobadilishwa na na idadi ya wanaosikia njaa kila siku zitakapopungua, bila shaka tutawahi kuadhimisha siku nyingi za chakula duniani katika miaka ijayo.