1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Seoul. Mateka 19 wawasili nyumbani.

2 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBTX

Raia 19 wa Korea ya kusini ambao walikuwa wakishikiliwa mateka kwa muda wa wiki sita na kundi la wapiganaji wa Taliban nchini Afghanistan wamewasili nyumbani.

Watu hao 19 , ambao waliachiwa huru kwa mafungu wiki iliyopita , wamewasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Seoul wakitokea Dubai.

Walikuwa miongoni mwa kundi la wafanyakazi 23 wa kutoa misaada wa kanisa la Kikristo ambao walikamatwa na wapiganaji wa Taliban karibu na mji wa kusini nchini Afghanistan wa Kandahar katikati ya mwezi Julai.

Taliban waliwauwa wawili kati ya mateka wanaume katika siku za mwanzo za mzozo huo, baada ya serikali ya Afghanistan kushindwa kutimiza madai ya wapiganaji hao ya kutaka wenzao walioko jela waachiliwe huru.

Wapiganaji hao baadaye waliwaachia mateka wawili wanawake katika kile walichokieleza kuwa ni kuonyesha nia njema.

Wakati huo huo , serikali ya Korea ya kusini imekanusha ripoti za vyombo vya habari kuwa imelipa milioni kadha za Euro kama kikomboleo cha kuwaachia mateka hao. Waziri wa mambo ya kigeni wa Korea ya Kusini Song Min Soon amesema jana kuwa serikali ilijaribu kila inalowezekana kuokoa maisha ya raia wake.

Tumejaribu kwa uwezo wetu kutumia misingi na kanuni za kimataifa , wakati ambapo tumekuwa tukitilia maanani zaidi maisha ya mateka hao.