1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Senegal Abdoulaye Wade, ataka Shirika la FAO kuvunjwa

5 Mei 2008

Rais wa Senegal Abdoulaye Wade, ametoa wito kwa Umoja wa Mataifa-UN, kulivunja Shirika la Kimataifa la Kilimo na Chakula-FAO.

https://p.dw.com/p/Dtxr
Rais wa Senegal Abdoulaye Wade.Picha: AP

Rais Wade amesema kuwa Shirika hilo linapoteza fedha na kulishutumu kuwa limeshindwa kusaidia kuzuia tatizo la chakula ulimwenguni.

Shirika la Kimataifa la Kilimo na chalakula-FAO lenye makao yake makuu Roma, linaongozwa na Raia kutoka Senegal Jacques Diouf ambaye rais Wade amesema alisaidia kuchaguliwa kwake.

Katika taarifa yake aliyoitoa jana, Rais Wade alisema mbali na Utendaji mzuri alio nao Mkurugenzi wa FAO, lakini ni Shirika lenyewe ndilo lenye matatizo.

Hata hivyo mpaka sasa FAO, hawajazungumzia chochote kuhusiana na pendekezo hilo la Rais Wade kwamba FAO haifanyi chochote na badala yake inapoteza fedha.

Msemaji wa FAO, Nick Parsons, ameliambia Shirika la Habari la Ufaransa-AFP kwamba Kama Shirika hawana cha kuzungumzia kwa sasa.Lakini mtu anayetarajiwa kuzungumza pengine chochote kuhusu pendekezo hilo ni Mkurugenzi wa FAO, Jacques Diouf.

Rais Wade alisema kuwa FAO imekuwa ikipoteza fedha nyingi kwa kutumia muda mwingi kwenye miradi midogo ambayo haikuleta mafanikio yoyote.

Aidha ameshutumu pia Ongezeko la bei za Nafaka ulimwenguni kuwa linasababishwa na uzembe wa FAO.

Rais Wade amesema kwa muda mrufu sasa ameekuwa akifanya kampeni kwa Shirika la FAO kuendelea kuifanya Afrika kuwa masikini kutokana tatizo la upungufu wa chakula na njaa.

Amesema kwa sasa ataenda mbali zaidi katika kampeni hiyo na kwamba ni lazima livunjwe na kuongeza kuwa kazi za FAO zimekuwa zikifanywa na Mashirika mengine vizuri zaidi kuliko FAO yenyewe.

FAO iliomba msaada wa dola milioni moja nukta saba kwa ajili ya mradi wake wa dharura wa kugawa mbegu na mbolea ili mazao ya kilimo yaweze kuongezeka wakati huo huo Shirika lingine la Umoja wa Mataifa la kuendeleza Kilimo,IFAD, liliahidi kutoa dola milioni miambili kuwasidia wakulima masikini waliko katika nchi zilizoadhirika zaidi.

Amesema kuna tofauti kubwa kati ya mapendekezo hayo mawili na inaonyesha ni jinsi gani FAO inavyozidi kutengwa.

Rais Wade amefafanua kuwa IFAD, ambayo inashughulikia masuala ya kuzuia umasikini na njaa katika maeneo ya vijijini kwenye nchi zinazoendelea kupitia mikopo na misaada, inaweza kuwa msaada mkubwa wa kuendeleza kilimo ulimwenguni kupitia makao makuu yake yaliyoko Afrika.

Hata hivyo Wachambuzi wa mambo wanaamini kwamba tatizo hili la chakula lilikuwa likingojewa kutokea kwa sababu ulaji umekuwa mkubwa zaidi kuliko uzalishaji wa mazao.

Akizungumzia Tatizo la upungufu wa chakula duniani hivi karibuni katika ufunguzi wa Mkutano wa Shirika la biashara na maendeleo la Umoja wa Mataifa Katibu Mkuu wa Umoja huo Ban Ki-Moon, alisema tatizo la njaa halikusabishwa na kupanda kwa bei za vyakula pekee bali pia mabadiliko ya hali ya hewa na mafuta kupanda.

Kwa mujibu wa wachambu, suluhisho pekee la hali iliyopo kwa sasa ni uwekezaji mkubwa katika kilimo.