1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Sarkozy ziarani Libya

Mohammed Abdul-Rahman25 Julai 2007

Ni kuimarisha mafungamano mapya ya kisiasa na kiuchumi na taifa hilo la Afrika kaskazini lenye utajiri wa mfuta.

https://p.dw.com/p/CB2T
Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy
Rais wa Ufaransa Nicolas SarkozyPicha: AP

Ziara hii ya rais Sarkozy inakuja baada ya Ufaransa kusaidia kuachiwa huru wahudumu sita wa kigeni wa sekta ya afya ambao kukamatwa kwao tangu 1999 kwa kuwaambukiza watoto 400 damu iliokua na virusi vya ukimwi, kuliuzorotesha zaidi uhusiano wa nchi za magharibi na Libya.

Kiongozi huyo wa Ufaransa amesema anataka kuisaidia Libya irudi katika jamii ya kimataifa baada ya kutengwa kwa zaidi ya miongo mitatu kwa sababu ya shutuma za nchi za magharibi kwamba ikiunga mkono ugaidi. Lakini pamoja na hayo atachukua nafasi hiyo kuyapa msukumo masilahi ya kitaifa ya Ufaransa katika uwanja wa biashara pamoja na kutanua ushawishi wa Ufaransa katika safu ya diplomasia barani Afrika.

Uhusiano baina ya Ufaransa na Libya uliharibika baada ya shambulio la ndege ya abiria ya Ufaransa 1989. Ufaransa ikawakuta na hatia walibya sita wakiwa wenye hawako nchini humo, lakini Libya ikakanusha kuhusika na hujuma hiyo. Uhusiano ulianza kuboreka pale nchi za magharibi zilipoondoa vikwazo dhidi ya Libya 2003 na Libya kwa upande wake kuachana na mradi wa silaha za maangamizi.

Sarkozy aliizuru Libya mwaka jana akiwa waziri wa ndani, lakini suala la wauguzi watano wakibulgaria na daktari wa kipalestina, likawa kikwazo katika kurejeshwa kwa uhusiano wa kawaida kati ya Ufaransa na Libya. Ufaransa ilifanikisha kuachiwa kwao, wakati mke wa Sarkozy , Cecilia Sarkozy alipokwenda Libya akijiunga na mjumbe wa umoja wa ulaya na hatimae wahudumu hao sita wa sekta ya afya kuachiwa huru jana baada ya kuwa gerezani kwa miaka 8.

Huenda Ufaransa ikawa na azma ya kuingia katika soko la Libya katika kuiuzia silaha na hasa ndege zake za kivita, pamoja na kukuza benki za fedha za Ufaransa. Maafisa wa Libya wamesema akiwa Tripoli Sarkozy anatarajiwa kusaini mikataba ya ushirikiano katika masuala ya usalama, nishati, elimu, uhamiaji, afya na utafiti wa kisayansi.

Ziara ya rais Sarkozy nchini Libya itafuatiwa na ziara ya kwanza kusini mwa Jangwa la sahara tangu achaguliwe kuwa rais mwezi mei, ambapo atazizuru Senegal kesho na baadae Gabon makoloni ya zamani ya Ufaransa. Katika ujumbe wake yumo pia waziri wake wa mambo ya nchi za nje Bernard Kouchner.