1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Robert Mugabe ajiuzulu

John Juma
21 Novemba 2017

Rais Mugabe hatimae amejiuzulu. Shangwe na nderemo zimerindima katika mitaa ya mji mkuu Harare huku waliojitokeza wakisikika wakiimba nyimbo za kumsifia mkuu wa majeshi, Chiwenga kufuatia tangazo la kujiuzulu kwa Mugabe

https://p.dw.com/p/2o0m9
Simbabwe Mugabe bei TV-Ansprache
Picha: picture-alliance/AP Photo

Hatimae rais Robert Mugabe wa Zimbabwe amejiuzulu. Amechukua hatua hiyo muda mfupi tu baada ya bunge kuanza mchakato wa kumuondoa madarakani. Hatua yake inatia kikomo utawala wake ambao umedumu kwa miaka 37.

Mugabe mwenye umri wa miaka 93, aliendelea kung'ang'nia madaraka kwa wiki moja tangu jeshi kuchukua udhibiti wa mamlaka na pia baada ya chama tawala cha ZANU-PF kumtaka aondoke madarakani.

Sherehe Harare kufuatia kujiuzulu kwa Mugabe

Kumetokea sherehe katika kikao cha pamoja cha bunge na seneti pale Spika Jacob Mudenda alipotangaza kuwa Mugabe amejiuzulu, na hivyo akauvunja mchakato huo uliokuwa ukiendelea wa kumvua Mugabe madaraka. Shangwe na nderemo zilirindima katika mitaa ya mji mkuu Harare huku waliojitokeza wakisikika wakiimba nyimbo za kumsifia mkuu wa majeshi,Chiwenga.

KIkao cha pamoja cha bunge na seneti kilichokuwa kikiendeleza mchakato wa kumvua madaraka Mugabe
KIkao cha pamoja cha bunge na seneti kilichokuwa kikiendeleza mchakato wa kumvua madaraka MugabePicha: Reuters/A. Ufumeli

Chama cha maveterani wa vita vya ukombozi wa nchi hiyo kimekuwa kikimshinikiza Mugabe ajiuzulu. Aidha wabunge na wanaharakati wa kutetea haki za binadamu  pia wamekuwa wakitoa wito kwa Mugabe ajiuzulu, huku maelfu kwa maelfu ya raia wakijitokeza kuandamana mjini Harare dhidi ya Mugabe.

Jeshi lilitwaa mamlaka wiki iliyopita, baada ya Mugabe kumfuta kazi aliyekuwa makamu wake Emmerson Mnangagwa, kama hatua ya kutengeneza njia kwa mke wake Grace mwenye umri wa miaka 52 kumrithi kiti cha urais.

Kiini cha kuanguka kwa Mugabe kimejikita katika ushindani kati ya washawishi wa ndani ya chama tawala wanaotaka kumrithi.

Mnangagwa, ambaye ni mkuu wa zamani wa usalama na anayejulikana kwa jina la utani la Mamba anatarajiwa kuchukua uongozi kama rais.

Mwandishi: John Juma/RTRE

Mhariri:  Yusuf Saumu