1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis atimiza mwaka madarakani

Oumilkher Hamidou13 Machi 2014

Baada ya kukabidhiwa uongozi wa kanisa katoliki ulimwenguni mwaka mmoja uliopita, Papa Francis ametuliza nyoyo za waumini wengi, na bila ya kufanya mapinduzi amebadilisha desturi na mitindo iliyokuwa ikiendelea Vatikan.

https://p.dw.com/p/1BOwp
Papa Francis ambaye ametimiza mwaka 1 tangu achaguliwe kuchukua wadhifa huo.
Papa Francis ambaye ametimiza mwaka 1 tangu achaguliwe kuchukua wadhifa huo.Picha: Reuters

Akiwa Papa wa kwanza anaetokea bara la Amerika Kusini, muumini wa kwanza wa kutoka shirika la Jesuiti kukabidhiwa hatamu za uongozi wa kanisa katoliki ulimwenguni na pia kiongozi wa kwanza wa kanisa kuwa na mpango maalum uliopewa jina Francis. Sifa zote hizo zinaonyesha hali ya aina pekee ya mchamungu huyu anaetokea Argentina.

Tangu mwaka mmoja uliopita, yaani Machi 13 usiku mwaka 2013 yeye ndie anaeongoza kanisa katoliki ulimwenguni kwa jina Papa Francis.

Hajakawia kutuliza nyoyo za waumini kuanzia wale walioko Vatikan hadi katika maeneo ya mbali kabisa duniani. Papa Francis anafuata utaratibu wake mwenyewe utaratibu unaobainisha jinsi yeye binafsi anavyotathmini wadhifa wa kiongozi wa kanisa katoliki ulimwenguni.

Mnyenyekevu tangu mwanzo

Kuanzia siku ya mwanzo tu alipohutubia kutoka roshani ya kanisa kuu la mtakatifu Petro watu waligundua jinsi alivyokuwa akishadidia yeye ni "Askofu mkuu wa Roma." Hiyo ni mojawapo ya vyeo kadhaa rasmi ambavyo kawaida hupatiwa kiongozi wa kanisa katoliki duniani.

Tangu alipochaguliwa Papa Francis ameonyesha kutopenda makuu
Tangu alipochaguliwa Papa Francis ameonyesha kutopenda makuuPicha: picture-alliance/dpa

Ni nadra kumuona Papa akishadidia mchango wake katika enzi hizi mpya tulizonazo. Mbele ya makanisa mengine,bila ya kujali madhehebu, hali hiyo huonekana kuwa ni sawa na kujishushia hadhi.

Na hakuna Papa yeyote wa enzi hizi tunazozijua aliyekuwa akijilinganisha sana na mchungaji. Francis anapenda sana kuwajongelea wananchi, jambo ambalo haliwafurahishi sana waumini huko Vatikan pamoja pia na vikosi vya usalama. Anapenda kuzungumzia yale ambayo watu wanapenda kuyasikia na ambayo yanawatuliza roho ingawa yanagusia masuala ya kidini pia.

Mtindo wa kipekee

Anafuatilizia namna hali za watu zilivyo. Sio tu kwa kufanya ziara ya mara kwa mara katika eneo la Lampedusa lililoko karibu na bara la Afrika au katika mitaa wanakoishi watu wasiojimudu mjini Roma. Katika mahojiano aliyoyafanya siku chache zilizopita ameelezea uzoefu wake wa kuwapigia simu watu wa kawaida na kuzungumzia mfano mmoja, mjane mwenye umri wa miaka 80 aliyefiwa na mwanawe wa kiume. Alimuandikia akisema ameamua kumpigia simu mara moja kwa mwezi.

Papa huyu amefanya juhudi kuyakaribia makundi yote ya watu
Papa huyu amefanya juhudi kuyakaribia makundi yote ya watuPicha: picture-alliance/dpa

Papa Francis anataka mengi zaidi; mageuzi, tangu makubwa mpaka madogo. Na mageuzi kama hayo simu haitoshi. Lakini Papa huyu wa kutoka Argentina anakumbusha yaliyotokea miaka 800 iliyopita katika enzi za yule anaefuata nyayo zake mshirika mwenzake Francis wa Asisi . Amehama kutoka kasri la kanisa na kuhamia katika nyumba anakoishi pamoja na wachamungu wengine.

Kila siku anahubiri ujumbe wa Biblia kwa kutumia lugha ya kawaida. Anakosoa hali mbaya inayozonga mfumo wa kiuchumi na kukaripia uzembe katika sera za kuwahudumia wakimbizi. Na hakuna anaetaharuki. Anawatafuta wanyonge, kuanzia wakimbizi, watu masikini na walemavu ambao huhudhuria kwa wingi anapohubiri katika uwanja wa mtakatifu Petro mjini Roma.

March 13 mwaka 2013 ni mwanzo wa enzi za mapinduzi. Nani aliyefikiria hali hii kabla ya kuitisha uamuzi wa kihistoria wa kustaafu Papa Benedikt wa 16 akiwa na umri wa miaka 86? Au Nani aliyefikiria kuwaona miezi michache iliyopita viongozi hao wawili mpya na wa zamani wamekumbatiana baada ya misa katika uwanja wa Mtakatifu Petro?

Mwandishi:Strack,Christoph/Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Yusuf Saumu