1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Benedict wa XVI aanza ziara ya Marekani

Kalyango Siraj16 Aprili 2008

Pia amealikwa Ikulu ya White House

https://p.dw.com/p/Dis0
Kiongozi wa dini ya Kikatoliki dunaini Papa Benedict XVI (katikati alievaa nguo nyeupe)akilakiwa katika uwanja wa ndege wa kijeshi wa Andrews Air Force Base Maryland, Jumanne, April 15, 2008.Picha: AP

Kiongozi wa dini Katoliki duniani Papa Benedict wa kumi na sita amewasili Marekani kwa ziara rasmi ya sita yenye shunguli nyingi.Alipokuwa njiani kuelekea huko kiongozi huyo wa kidini amegusia suala nyeti ambalo linaloikabili kanisa ya nchini aliko sasa la visa vya Mapadri kuwaingilia kimwili kwa nguvu watoto.

Hii ndio ziara ya kwanza ya Papa Benedict wa kumi na sita nchini Marekani tangu achukue hatamu za uongozi wa kanisi hilo miaka mitatu iliopita.Amelakiwa katika uwanja wa kijeshi wa Andrew Airforce Base Maryland, nje ya jiji la Washington na mwenyeji wake rais Gerorge W Bush,mkewe Laura Bush pamoja na bint wao Jenna Bush.

Hii ndio mara ya kwanza kwa rais Bush kumlaki mgeni yeyote wa nje katika uwanja wa ndege.Ziara yake hii inagubikwa na kashfa ya mapadri wa kanisha hilo nchini Marekani ambao wanalaumiwa kwa kuwanyanyasa watoto.Madai yamekuwa yakisikika kuwa baadhi ya mapadri wamekuwa wakiwaingilia kimwili kwa nguvu watoto wa kiume. Suala hilo inaonekana lilikuwa linamfanya atakune kichwa, na kumbidi akiwa njiani aseme kuwa anasikitishwa sana na visa hivyo.

Aidha ameapa kuwaondoa mapadri waovu kutoka katika kazi ya Mungu.Rais Bush na Papa Benedict wamepangiwa kukutana leo jumatano kwa dhifa ya kitaifa na baadae kufanya mazunguzo ya faragha katika ikulu ya White-House.Hii itakuwa mara ya pili kiongozi wa kidini akitembelea ikulu hiyo.

Ni viongozi watatu wa dini katoliki duniani ambao wametembelea Marekani wa kwanza akiwa Papa Yohana Paulo wa 6 mwaka wa 1965.

Hayati Papa John Paulo wa pili alizuru Marekani mara saba na ziara yake ya mwisho ilikuwa mwaka wa 1999 katika eneo la St.Louis mjini Missouri.Ingawa alifanya mikutano sita na marais wa Marekani,lakini alitembelea ikulu ya White house mara moja tu, mwaka wa 1979 na baada ya kualikwa na rais Jimmy Carter.

Marekani ilianzisha uhusiano wa kidplomasia na Vaticana mwaka wa 1984.

Mbali na ziara hii nchini Marekani lakini kwa wakati huu kiongozi huyo wa dini katoliki anaadhimisha miaka 81ya kuzaliwa leo jumatano.Kwa mantiki hiyo ameandaliwa karamu murua katika ikulu ya Marekani. Takriban watu kati ya 9,000 na 12,000 wakiwemo watawa,waumini wa kawaida pamoja na watoto,ndio wamealikwa kuhudhuria karamu hiyo.

Na rais Bush anategemewa kutumia nafasi hiyo kumwambia kiongozi wa kidini pamoja na umati wa wageni waalikwa katika karamu kuwa Marekani inafurahia ziara yake hii.

Na kwa upande mwingine rais Bush anatarajiwa pia kuwaomba raia wa Marekani kusikiliza maneno ya kiongozi huyo.

Papa Benedict nae anatarajiwa kuzusha mjadala wa masuala nyeti katika safari yake hii.Miongoni mwa masuala hayo ni vita vya Iraq pamoja na suala la uhamiaji.

Kuhusu vita vya Iraq ambavyo vimesababisha wanajeshi wa Marekani zaidi ya 4,000 kupoteza maisha yao hadi sasa.Na mtangulizi wa Papa Benedict,Yohanna Paulo wa pili alivipinga.

Suala la uhamiaji anaweza kulijadili kufuatia kamatakamata ya serikali ya Marekani dhidi ya wahamiaji kutoka Amerika ya Kusini.

Marekani inasema inawatafuta tu wahamiaji haramu.

Watu wanaoongea Kihispania nchini Marekani, wanakadiriwa kuunda asili mia 40 ya wafuasi wa dini katoliki nchini humo wanaofikia millioni 70.