1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama amlaumu Assad kupoteza fursa ya mageuzi

13 Julai 2011

Rais Barack Obama wa Marekani amesema Rais Bashar Al-Assad wa Syria ameshapoteza fursa muhimu za kuleta mageuzi katika nchi yake na sasa kiongozi huyo anayekabiliwa na maandamano anapoteza uhalali mbele ya raia wake.

https://p.dw.com/p/11tvl
Rais Barack Obama wa Marekani
Rais Barack Obama wa MarekaniPicha: AP

Akizungumza na kituo cha televisheni cha CBS, Rais Obama pia ameyalaani mashambulizi dhidi ya ubalozi wa Marekani mjini Damascus. Rais Obama amesema nchi yake imeipelekea serikali ya Syria ujumbe wa wazi kwamba "haiwezi kuvumilia uvamizi wa balozi zake" na kwamba ni jukumu la serikali hiyo kutoa ulinzi wa uhakika kwa balozi za kigeni nchini mwake.

Wakati huo huo, msemaji wa wizara ya nje ya Marekani, Victoria Nuland, amesema balozi wa Marekani mjini Damascus, Robert Ford, amekutana na naibu waziri wa mambo ya nje wa Syria kwa mazungumzo yaliyotajwa kuwa ya "ushirikiano."

Hapo jana (12 Julai 2011), Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, lililaani vikali kushambuliwa kwa balozi za Marekani na Ufaransa nchini Syria kulikofanywa na watu wanaoshukiwa kuwa wafuasi wa Rais Assad hapo Jumatatu.

Mwandishi: Mohammed Khelef/AFP
Mhariri: Sekione Kitojo