1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ni upande upi wa Madrid utajigamba?

Bruce Amani
2 Mei 2017

Real Madrid wanapambana na Atletico Madrid katika mchuano wa mkondo wa kwanza wa nusu fainali ya Champions League. Ni mchuano utrakaokuwa na hisia kali maana timu zote mbili zinafahamiana vyema kabisa

https://p.dw.com/p/2cEmx
Symbolbild Cristiano Ronaldo und Antoine Griezmann
Picha: picture alliance/dpa/L. Jr - Kiko Huesca

Real waliizaba Atletico katika misimu yote mitatu waliyocheza dimba hilo, ikiwa ni mara mbili katika fainali iliyowapa kilio Atletico mwaka wa 2014 na 2016.

Nahodha wa Atletico Gabi amesisitiza kuwa kinachompa motisha ni kushinda Champions League na sio kutafuta kulipiza kisasi dhidi ya Real Madrid.

Timu zote mbili zinatafuta ushindi wa kihistoria huku Real wakilenga kupata ubingwa wa 12 wa Ulaya katika fainali ya Cardiff mnamo Juni 3 kwa kuwa timu pekee ya kwanza kuhifadhi Kombe hilo tangu dimba la Champions League lilipozinduliwa.

Wakati huo huo Atletico wangali wanatauta kushinda taji lao la kwanza kabisa la Champions League wakiwa timu pekee kushindwa katika fainali tatu bila kuwahi kubeba kombe hilo.

Gareth Bale na beki wa kati Pepe ndio wachezaji pekee wa Real watakaoachwa nje ya kikosi kwa mchuano wa leo. Isco na Marco Asensio watatumiwa kuijaza nafasi ya Bale, wakati Raphael Varane atachukua nafasi ya Pepe katika mabadiliko pekee ambayo kocha Zinedine Zidane anatazamiwa kufanya.

Kocha Diego Simeone hivyo basi atalazimika kufanya mabadiliko katika safu ya ulinzi kwa kumtumia Stefan Savic, huku Lucas Hernandez akishirikiana na Godin katika ngome ya ulinzi.

Yannick Carrasco pia huenda asiweze kucheza baada ya winga huyo Mbelgiji kuumia wiki jana. Kurejea kwa Kevin Gameiro, hata hivyo ni habari nzuri kwa kocha Simeone.

Mwandishi: Bruce Amani/AP
Mhariri: Iddi Sessanga