1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NEW YORK : Madaraka zaidi kwa Waziri Mkuu Ivory Coast

2 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCws

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hapo jana limeidhinisha kwa kauli moja kumpa madaraka makubwa ya utendaji Waziri Mkuu wa Ivory Coast Konan Banny kuongoza serikali ya mpito kuelekea uchaguzi mkuu mpya katika nchi hiyo iliogawaika ya Afrika Magharibi.

Joreg Voto- Bernales balozi wa Peru katika Umoja wa Mataifa ambaye ni Rais wa Baraza la Usalama kwa mwezi wa Novemba ametangaza kwamba nchi zote 15 wanachama wa baraza hilo zimeunga mkono azimio lililorasimiwa na Ufaransa ambalo pia linaidhinisha uamuzi wa Umoja wa Afrika wa kuendelea kuwaweka Konnan Banny na Rais Laurent Gbagbo katika nyadhifa zao kwa kipindi kipya cha serikali ya mpito kisichopindukia miezi 12.

Balozi wa Ivory Coast katika Umoja wa Mataifa Philippe Djangons –Bi amesisitiza kwamba azimio hilo halimaanishi kwamba katiba ya nchi hiyo imekiukwa na kwamba Gbagbo inabidi aachie madaraka yake yote kwa Konan Banny.

Amesema waziri mkuu huyo atapewa madaraka yale ambayo yanahitajika tu kwa ajili ya kuiongoza nchi hiyo kwenye uchaguzi.

Azimio hili kimsingi linakusudia kuwapokonya silaha wanamgambo,kuandaa uchaguzi ambao tayari umeahirishwa mara mbili tokea mwaka 2004 na kuiunganisha tena nchi hiyo iliogawika pande mbili tokea kushindwa kwa jaribio la kumpinduwa Gbagbo hapo mwezi wa Septemba mwaka 2002.