1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Netanyahu ziarani India

Sekione Kitojo
14 Januari 2018

Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliwasili  nchini India Jumapili kwa ziara ya kwanza ya kiongozi wa Israel  nchini India katika muda wa miaka 15, akiahidi mahusiano ya karibu na taifa hilo.

https://p.dw.com/p/2qp9Y
Jerusalem - Israelischer Premierminister Benjamin Netanyahu und  indischer Premierminister Narendra Modi
Picha: picture-alliance/AP Photo/S. Scheiner

Netanyahu  na  mkewe Sara walilakiwa  katika  uwanja  wa  ndege wa  kimataifa mjini  New Delhi  na  waziri  mkuu Narendra Modi ambaye aliandika  historia  mwezi Julai  baada  ya  kuwa  kiongozi wa  kwanza  wa  India  kuizuru Israel.

"Ziara  hiyo ni  fursa  ya  kuimarisha  ushirikiano katika  nguvu ya uchumi  wa  dunia , usalama, teknolojia na  uwezo  wa  kiutalii," Netanyahu  alisema  katika  taarifa  kabla  ya  ziara  hiyo.

Jerusalem - Israelischer Premierminister Benjamin Netanyahu und  indischer Premierminister Narendra Modi
Waziri mkuu Narendra Modi wa India (kushoto) na waziri mkuu wa Israel NetanyahuPicha: picture-alliance/AP Photo/S. Scheiner

"Waziri  mkuu  wa  India Modi ni  rafiki  wa  karibu  wa Israel  na mimi."

Modi ambaye  atafuatana  pamoja  na  Netanyahu katika  sehemu kubwa  ya  ziara  hiyo  ya  siku  tano , alikumbatiana  na  waziri mkuu  wa  Israel mara  baada  ya  kuwasili  kabla ya  viongozi  hao wawili  kutoa heshima zao katika  eneo  la  kumbukumbu  ya  vita katika  mji  huo  mkuu  wa  India.

"Ziara yako  nchini  India  ni  ya  kihistoria  na maalum. itaimarisha zaidi  urafiki  wa  karibu  baina  ya  mataifa  yetu," alisema  Modi kupitia  ukurasa  wa  Twitter.

Netanyahu atakuwa ni  waziri  mkuu  wa  pili  wa  Israel  kuitembelea India baada ya Ariel Sharon  kufanya  hivyo mwaka  2003.

Ujumbe  wa makampuni ya biashara

Anafuatana  na  ujumbe  mkubwa  kabisa  wa  kibiashara  kuwahi kusafiri  na  kiongozi  wa  Israel. Viongozi  wakuu  wa  makampuni ya  teknolojia , kilimo  na  ulinzi  ni  miongoni  mwa  waliomo  katika msafara  huo  wakati  Israel  inatafuta  makubaliano  na  taifa  hilo lenye  uchumi  mkubwa  wa  tatu  katika  bara  la  Asia.

Premierminister Indien Narendra Modi
Waziri mkuu wa India Narendra ModiPicha: Getty Images/AFP/P. Singh

Hatua  za  kuelekea katika  ziara  ya  Netanyahu  zilichafuka  mwezi huu wakati  India  ilipositisha  makubaliano  ya  kununua makombora yanayolenga vifaru  kutoka  kampuni  inayomilikiwa  na  serikali  ya Israel  ya kandarasi  ya  masuala  ya  ulinzi Rafael.

Jeshi la  India  na  serikali vinajadili  njia  za  kufufua  maombi ya dola  milioni 500, ambayo  yalifutwa wakati  kampuni  ya kandarasi ya  masuala  ya  ulinzi  inayomilikiwa  na  serikali  ilipendekeza kutengeneza  makombora  kama  hayo  nchini  humo.

Israel  ni muuzaji  mkuu  wa  sihala  nchini  India , ikiuza nje  wastani wa  vifaa  vya  kijeshi  vinavyofikia  thamani  ya  dola  bilioni 1 kila mwaka, lakini  Modi  anataka  kufikisha  mwisho   hali  ya  India kuwa  ni mnunuzi  mkubwa  wa  vifaa  vya  ulinzi  duniani.

Netanyahu  na  Modi  walianza  ziara  hiyo  kwa  kutembelea kumbukumbu  ya  wanajeshi  wa  India  waliopigana  katika  vita vikuu  vya  pili  vya  dunia katika  kusaidia  kuukomboa  mji  wa  Haifa nchini  Israel.

Makubaliano ya kibiashara

Kiongozi  huyo  wa  Israel baadaye atakutana  na  waziri  wa  mambo ya  kigeni  Shushma Swaraj kabla  ya  kupata  chakula  cha  usiku pamoja  na  waziri  mkuu  Modi  binafsi.

Netanyahu  anatarajiwa  kutia  saini  makubaliano  mapya  katika nyanja  za  nishati, usafiri  wa  anga  na  utengenezaji  wa  filamu , pia  atatembelea  jumba  la  Taj Mahal, atazuru  jimbo  anakotoka Modi  la  Gujarat  na  kukutana  na  wacheza sinema maafuru  wa Bollywood  mjini  Mumbai.

Check-in 20.05..2017. V-Mail
Jengo la Taj Mahal nchini IndiaPicha: DW

Lakini  pia atafanya  ziara  katika  kituo  cha  Wayahudi kilichoshambuliwa  mwaka  2008 mjini  Mumbai , ikiwa  ni  ishara  ya kuonesha mshikamano  na  jamii  ndogo  ya  Wayahudi  nchini  India ambayo  inazidi  kupungua.

Netanyahu atafuatana na  Moshe Holtzberg  mwenye  umri  wa miaka  11 wakati  kijana  huyo  akirejea  kwa  mara  ya  kwanza katika  nyumba  ambako  wazazi  wake waliuwawa  katika mashambulizi  hayo ambayo  yamesababisha  watu 166  kuuwawa.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Oummilkheir Hamidou