1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi za Afrika zinazidi kustawi

Sylvia Mwehozi
22 Mei 2017

Ripoti iliyotolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika, AfDB, kuhusu mustakabali wa ukuaji uchumi wa Afrika inaonesha kwamba Waafrika wengi wanaona kuna ustawi katika hali za maisha yao.

https://p.dw.com/p/2dMSH
Nov 27 2014 Cape Town South Africa View of the Gautrain inside Pretoria station Gautrain is
Picha: imago/ZUMA Press

Wakati idadi kubwa ya wakaazi wa bara la Afrika karibu watu bilioni 1.2 wanaishi katika umasikini, mataifa mengi kati ya 54 ya bara hilo yamepata mafanikio makubwa katika nyanja za afya, elimu na hali ya maisha.

"Angalau theluthi tatu ya nchi za afrika zimepata mafanikio ya kati ya viwango vya juu vya maendeleo ya binadamu", imesema ripoti hiyo ya AfDB, ikimaanisha mkusanyiko wa kipimo cha hali ya taifa.

Afrika Kaskazini ina kiwango cha juu, ikikaribiana na viwango vya kimataifa, ambapo Misri na Tunisia zinatajwa kuwa zina mfumo wa bima ya afya unaowafikia watu kwa asilimia 75 kati ya 100.

Pia kumeshuhudiwa mafanikio kadhaa katika mataifa mengine tangu kuanza kwa karne ya 21. Rwanda imetajwa kuwa nchi iliyopiga hatua zaidi katika mataifa yaliyo kusini mwa Jangwa la Sahara, ikifuatiwa na Ghana na Liberia, katika mapambano dhidi ya umaskini tangu mwaka 2005. Mojawapo ya jitihada kubwa za Rwanda, ilikuwa ni mfumo wa huduma ya bima ya afya ya kijamii ambapo hadi mwaka 2010, ilikuwa imewafikia watu tisa kati ya 10.

Japanese Prime Minister Shinzo Abe in Nairobi
Rais wa Rwanda Paul Kagame Picha: picture-alliance/dpa/D. Kurokawa

Matumizi katika elimu, suala ambalo linachukuliwa kuwa kigezo muhimu cha maendeleo limefikia juu ya asilimia sita ya pato la taifa nchini Afrika Kusini, Ghana, Msumbiji na Tunisia, lakini Nigeria, taifa lenye idadi kubwa zaidi ya watu barani humo, inatumia chini ya asilimia moja ya pato lake la ndani katika elimu.

Kwa mujibu wa takwimu za Benki ya Dunia, mataifa ya Umoja wa Ulaya yanatumia wastani wa asilimia 4.9 ya pato la taifa katika elimu kwa mwaka 2013.

Afrika ya Kati, ambako viwango vya kuhitimu shule kwa wasichana ni vya chini katika bara zima, pengo baina yao na wavulana linazidi kupungua. Idadi ya wasichana waliomaliza sekondari kwa mwaka 2014 imefikia mara tatu zaidi tofauti na muongo mmoja uliopita.

Usawa wa kijinsia umeongezeka katika mataifa kadhaa yakiwemo Botswana, Namibia, Rwanda ambako wanawake wanafikia viwango sawa vya maendeleo ya binadamu kama ilivyo kwa wanaume, imesema ripoti hiyo.

Ruanda Wirtschaftsforum in Kigali Akinwumi Ayodeji Adesina
Mkuu wa Benki ya maendeleo ya Afrika Akinwumi Ayodeji AdesinaPicha: World Economic Forum/Benedikt von Loebell

Licha ya hatua hizo, Waafrika milioni 544 wanaishi bado katika umaskini, imesema ripoti hiyo iliyopewa kichwa cha habari "Muonekano wa Kiuchumi wa Afrika mwaka 2017", ambapo bado changamoto nyingi zinasalia katika mapambano ya vita dhidi ya umaskini. Moja kati ya hizo ni ukosefu wa upatikanaji wa nishati ya kupikia, umeme na usafi wa mazingira. Watu milioni 645 kusini mwa Jangwa la Sahara wanaishi bila ya umeme.

Ripoti hiyo inasema kuwa mustakabali hauonekani kuwa mzuri kwa vijana wadogo ambao wengi wao hawana ajira, kutokana na vijana hao kupatiwa elimu isiyo na ujuzi sokoni.

Ripoti hiyo inatabiri kwamba yapo matumaini ya ukuaji wa uchumi kwa asilimia 3.4 kwa mwaka huu, ikiwa ni ongezeko baada ya kukua kwa asilimia 2.2 mwaka jana.

Afrika Mashariki inasalia kuwa ukanda ulio na nguvu kiuchumi kwa bara lote ikiongozwa na Ethiopia. Kwa ujumla Afrika iko nafasi ya pili katika ukuaji duniani kote nyuma ya mataifa yanayoendelea ya Asia.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AFP

Mhrairi: Mohammed Khelef