1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NAIROBI : Polisi yaendeleza msako wa Mungiki

6 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBuO

Polisi na wanajeshi wa kutuliza fujo wametumia viboko na gesi ya kutowa machozi katika mapambano na wakaazi wa kitongoji duni katika msako wa kundi la kihalifu la Mungiki wakati maiti moja iliokatwa kichwa kiwa imepatikana katika kitongoji hicho cha Nairobi wakati wa usiku.

Vurugu za jana usiku katika mtaa wa Mathare zimekuja baada ya polisi kuuwa takriban watu 22 katika mtaa huo alfajiri ya Jumanne katika jaribio la kuwasaka wanachama wa kundi hilo lililoteremsha balaa la mauaji na kukata watu vichwa katika mji wa Nairobi na eneo zima la Kenya ya kati.

Polisi iliwapiga risasi na kuwaua watuhumiwa wawili hapo jana usiku katika mtaa wa Mathare.

Kundi la polisi limeingia kwenye kitongoji hicho duni cha Mathare pia wakati wa mchana leo hii likivunja milango ya nyumba kwa mateke,kupinduwa mapipa ya pombe haramu ya kienyeji na kuwatia pingu watuhumiwa.

Mauaji hayo ya kundi hilo la Mungiki yamezusha hofu kwamba kundi hilo limekusudia kuvuruga uchaguzi uliopangwa kufanyika nchini Kenya hapo mwezi wa Desemba ambapo Rais Mwai Kibaki anatarajiwa kuwania kipindi cha pili madarakani.