1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NAIROBI: Mkutano waandaliwa nchini Kenya kuhusu mzozo wa Somalia.

5 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCd7

Maafisa wa kibalozi wa mataifa ya magharibi pamoja na Afrika wamekutana mjini Nairobi, Kenya kushauriana kuhusu kikosi cha kulinda amani na pia msaada kwa serikali ya Somalia ambayo imesaidiwa na Ethiopia kuwafurusha wanamgambo wa Kiislamu kutoka maeneo waliyokuwa wakidhibiti.

Kundi la Kimataifa linaloshughulikia Somalia , linalojumuisha Marekani na mataifa ya Ulaya, lilikuwa likishauriana na Rais wa Somalia, Abdullahi Yusuf, huku majeshi ya Somalia na Ethiopia yakikabiliana na mamia ya wanamgambo wa Kiislamu karibu na mpaka wa Kenya.

Kikosi cha wanamaji wa Marekani kimepiga kambi pwani ya Somalia kuzuia wanamgambo wa kiislamu kutoroka kupitia baharini.

Wakati huo huo, ukanda wa sauti unaosemekana umetoka kwa naibu kiongozi wa al Qaeda, Ayman al-Zawahiri, umewasilishwa kwenye mtandao ukiwataka wanamgambo wa Kiislamu nchini Somalia waanzishe mashambulio ya kuvizia kama ilivyo nchini Iraq dhidi ya majeshi ya Ethiopia nchini humo.