Mwandishi habari wa Ufaransa auawa Syria
12 Januari 2012Matangazo
Katika taarifa iliyotolewa mjini Paris, waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa, Alain Juppe vile vile amelaani kile alichokiita kitendo kinachokirihisha. Gilles Jacquier ni mwandishi habari wa kwanza wa nchi ya magharibi kuuawa nchini Syria, tangu maandamano dhidi ya Rais wa Syria Bashar al-Assad kuanza miezi 10 iliyopita.
Mwandishi habari huyo wa Kifaransa, ni miongoni mwa watu 8 waliouawa hapo jana, baada ya kujikuta katikati ya mapambano wakati wa kutembelea eneo hilo, baada ya kupata kibali cha serikali, ambalo ni jambo la nadra. Mwandishi habari wa Kiholanzi pia, ni miongoni mwa watu 25 waliojeruhiwa katika shambulio hilo. Syria imewapiga marufuku waandishi habari wengi wa kigeni tangu machafuko kuibuka nchini humo hapo mwezi Machi.