1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mvutano wa kisiasa nchini Ivory Coast.

Abdu Said Mtullya23 Desemba 2010

Mvutano unazidi kuwa wa hatari nchini Ivory Coast.

https://p.dw.com/p/zokX
Wananchi wa Ivory Coast katika mvutano wa kisiasa baada ya uchaguzi wa rais.Picha: Picture-Alliance/dpa

Waziri Mkuu wa upande wa upinzani unaotambulika kuwa mshindi wa uchaguzi nchini Ivory Coast bwana Guillaume Soro ametoa mwito kwa mahakama ya kimataifa ya ICC wa kupeleka ujumbe ili kushughulikia uhalifu unaotendeka kutokana na mvutano wa kisiasa nchini.Bwana Soro ametoa mwito huo leo wakati mvutano wa kisiasa unaendelea kuwa wa hatari nchini Ivory Coast.

Bwana Soro ambae ni waziri Mkuu wa kiongozi wa upinzani Alassane Outtara anaetambulika na Umoja wa Mataifa kuwa mshindi wa uchaguzi wa rais nchini Ivory Coast amesema anasubiri Mahakama ya Kimataifa inayopambana na uhalifu,ICC ipeleke ujumbe nchini Ivory Coast ili kuwabaini watu binafsi wanaohusika na uhalifu, na wote wengine watakaohusika, kwa namna yoyote, ili wapelekwe mbele ya mahakama hiyo mjini the Hague.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa watu, 50 wameshauawa nchini Ivory Coast tokea mvutano wa kisiasa uanze, kufuatia uchaguzi wa rais uliofanyika mwezi novemba. Upande wa upinzani unaoongozwa na Alassane Outtara unatambulika kuwa mshindi wa uchaguzi huo ,wakati rais wa hadi sasa Laurent Gbagbo alitangazwa kuwa mshindi Gbagbo anang'ang'ania madarakani licha ya miito kutolewa na jumuiya ya kimataifa ya kumtaka aondoke.

Waziri Mkuu wa upande wa upinzani Bwana Soro amesema anatumai kwamba jumuiya ya kimataifa haitachukua muda mrefu kutambua kuwa mahala ambapo Gbagbo anastahili kuwapo ni mbele ya mahakama ya ICC na siyo kwenye kasri ya rais.

Ivory Coast haijatia saini mkataba wa sheria wa Roma ulioanzisha mahakama ya ICC lakini Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linaweza kuchukua hatua ya kuwachunguza wanaotuhumiwa kutenda uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu.Na mwendesha mashataka mkuu wa mahakama ya ICC bwana Ocampo amesema mahakama hiyo itamfungulia mashtaka yeyote atakaeyashambulia majeshi ya Umoja wa Mataifa yanayolinda amani nchini Ivory Coast.

Wakati huo huo kamati ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia hati za utambulisho imemtambua balozi aliependekezwa na Alassane Outtara.Hiyo ni hatua nyingine ya jumuiya ya kimataifa ya kuendelea kumshinikiza rais Gbagbo ili ang'atuke.

Wakati mvutano unazidi kuwa mkubwa nchini Ivory Coast unaoweza kusababisha vita vingine vya wenyewe kwa wenyewe Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeongeza idadi ya wanajeshi wa Umoja huo wanaolinda amani nchini Ivory Coast hadi 10,000 na pia limerefusha kwa miezi sita muda wa kuwapo majeshi hayo nchini humo.

Wakati huo huo Marekani, pamoja na Ufaransa na nchi za Afrika, inatafakari hatua za kuliimarisha jeshi la Umoja wa Mataifa nchini Ivory Coast.

Mwandishi/Mtullya Abdu/AFPE/RTRE/

Mhariri/Josephat Charo