1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mourinho: kuna mkono wa mtu dhidi ya timu yangu

29 Desemba 2014

Kocha wa Chelsea Jose Mourinho anadai kuna kampeni ya kuwaadhibu wachezaji wake baada ya pambano lililomalizika kwa sare yagoli moja kwa moja dhidi ya Southampton.

https://p.dw.com/p/1EC0E
Campions League Schalke 04 gegen FC Chelsea
Kocha wa Chelsea MourinhoPicha: picture-alliance/dpa

Manuel Pellegrini kocha wa Manchester City amewashutumu wachezaji wake kwa kuridhika baada ya kupata mabao mawili dhidi ya Burnley na hatimaye kupoteza ushindi huo kwa mabao mawili ya kirahisi na kuwa sare ya mabao 2-2, ambayo inaiweka timu hiyo katika nafasi ngumu bado ya kuweza kuipiku Chelsea katika kinyang'anyiro cha kuwania ubingwa wa Ligi kuu ya Uingereza.

Mabingwa hao watetezi walipoteza fursa ya kusogea hadi pointi moja nyuma ya Chelsea , timu inayoongoza hivi sasa katika Premeir League, ambao nao Chelsea walikabwa koo na Southampton mapema jana Jumapili, na kutoka sare ya bao 1-1.

Huenda baada ya kuongoza kwa mabao 2-0 tulifikiri kila kitu kimemalizika lakini hadi inapolia firimbi ya mwisho, mchezo bado haujamalizika. Hatukuweza kuendelea na kasi ile ile.

Arsenal-Trainer Arsene Wenger mit Champions-League Pokal
Arsene Wenger kocha wa ArsenalPicha: picture-alliance/dpa

Pellegrini ambaye amefichua kuwa amemuweka kando Yaya Toure kwa tahadhari baada ya mchezaji huyo wa kimataifa wa Cote D'Ivoire kuripoti kuwa ana maumivu kidogo katika paja, aliendelea kubisha kuhusu nafasi finyu ya Manchester City kuchukua ubingwa mara hii licha ya kikwazo ilichokipata.

Nae kocha wa Chelsea Jose Mourinho amedai kwamba kuna kampeni ya kuwaadhibu wachezaji wake kwa kujirusha kufuatia timu yake kutoka sare ya bao 1-1 jana na Southampton.

Mchezaji wa kati wa Chelsea Cesc Fabregas alipewa kadi ya njano baada ya kuanguka wakati akikabiliana na Matthew Targett katika kipindi cha pili. Marudio ya picha za televisheni zimeonesha kwamba mwamuzi alifanya makosa , wakati Targett alionekana kumuwekea mguu Fabregas na kuanguka , lakini Mourinho amesema kuna kitu zaidi ya hicho.

Kocha wa Arsenal , Arsene Wenger amesema kikosi chake kinapata kasi katika wakati muafaka baada ya kuimarisha matumaini yao ya kufuzu kucheza katika Champions League mwakani kwa ushindi wa mabao 2-1 jana Jumapili dhidi ya West Ham United. Champions League ni muhimu kwetu, amesema Wenger . Tumeweza kushiriki kwa miaka 17 kwa hiyo nina haki kuamini kwamba tunaweza kufuzu.

Ukiangalia msimamo wa ligi , kila timu inapambana kwa nguvu zote kupata nafasi hiyo. Southampton, Tottenham, Man United, timu nyingi zinapambana kupata nafasi hiyo.

Mwandishi : Sekione Kitojo / afpe / rtre / dpae
Mhariri: Idd Ssessanga