1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa kilele wa G8 na madawa ya kuimarisha misuli

Oummilkheir31 Mei 2007

Jee mkutano wa kilele wa G8 utaleta tija na vipi kuwaandamana wanaspoti wanaotumia madawa ya kuimarisha misuli?

https://p.dw.com/p/CHSp

Mkutano wa kilele wa G8 na mjadala wa baraza la mawaziri kuhusu madawa wanayotumia wanaspoti kuimarisha misuli ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.

Tuanze basi na mkutano wa kilele wa jumuia ya nchi tajiri kwa viwanda G8.Ajenda ya mkutano huo ni ndefu lakini matumaini ya kufikiwa aina fulani ya makubaliano ni haba pakiwepo hofu kubwa pia za kuzuka maandamano mkutano wa viongozi wa nchi tajiri kabisa wa dunia hii utakapoitishwa siku sita kutoka sasa mjini Heiligendamm.Mawaziri wa mambo ya nchi za nje wa jumuia hiyo wamekutana mjini Postdam kuandaa mkutano huo wa kilele.Gazeti la WESTDEUTSCHE ZEITUNG linaandika:

“Mkutano huo wa kilele mtu anaweza kusema utashindwa tuu licha ya malengo hafifu iliojiwekea Ujerumani kama mwenyekiti wa G8.Bila ya shaka faida inapatikana kwa vyovyote vile pale wababe wa dunia wanapokutana na kubadilishana maoni.Lakini hali hiyo inatosha kweli kufidia jinsi sheria msingi zinavyofumbiwa macho?Sote tunajua kwamba “wapenda mashaka wakubwa” wa dunia hii hawakutikani katika mahema yaliyoko katika fukwe za Mecklenburg-bali ndani ya Hoteli kubwa iliyozungushwa senyenge za jumuia ya kujihami ya magharibi NATO.Isingekua vibaya kama siku za mbele mkutano huu wa kilele ungekua unafanyika kama zamani pale viongozi walipokua wakikutana ukumbini karibu na mahala pa kuota joto.

Gazeti la RHEIN-NECKAR-ZEITUNG la mjini Stuttgart linaandika:

„Bila ya shaka ni ujinga kusema:ahaa,mkutano wa kilele unaofanyika chini ya ulinzi mkali kama huu hautaleta chochote cha maana.Kwasababu hatua za usalama lazma zichukuliwe viongozi wakuu wa dunia wanapokutana.Na hasa katika enzi kama hizi za sasa ambapo harakati za kigaidi hazikadiriki.Lakini kuwatenganisha moja kwa moja wawakilishi wa G8 na wananchi,ni ishara ya kihoro.Nyingi ya hatua za kinga zilizochukuliwa hazijalengwa kujikinga dhidi ya uwezekano wa kuzuka mashambulio ya kigaidi,bali dhidi ya waandamanaji.“

Tuigeukie hivi sasa mada ya pili magazetini.Baada ya wanaspoti mashuhuri wa mbio za baskeli kukiri wamekua wakitumia madawa ya kuimarisha misuli,imekua zamu ya baraza la mawaziri hivi sasa kuzungumzia kadhia hiyo inayochafua hadhi ya michezo.Waziri wa mambo ya ndani Wolfgang Schäuble anapanga kuviandama visa vya kueneza madawa ya kuimarisha misuli-lakini anapanga kuwanusuru wasihukumiwe wanaspoti wanaokutikana na hatia.Kuhusu suala hilo gazeti la Kölner Stadt-Anzeiger limeandika:

„Ikigundulikana lakini kama mwanaspoti wa kulipwa anajishughulisha pia na kuuza madawa ya kuimarisha misuli- basi hapo atakabiliwa na sheria kali za matumizi mabaya ya madawa .Sheria kama hiyo haina maana yoyote.Kwasababu chanzo pekee cha uchunguzi dhidi ya wanaotumia madawa ya kuimarisha misuli kinakutikana pale ushahidi wa mkojo unapoonyesha kama kweli ametumia madawaya hayo ya kuimarisha misuli na sio kwasababu ya dhana ya kumiliki idadi kubwa ya madawa au kufanya biashara ya madawa hayo yanayoimarisha misuli. Na hapo ndipo panapokutikana walakin katika kupambana na matumizi ya madawa ya kuimarisha misuli.La sivyo pasingehitajika fikra ya kuwatuma wapelelezi kuchunguza kama wanaspoti wametakasika au la.