1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa G7 waanza na msimamo mkali kwa Urusi

7 Juni 2015

Viongozi wa Ujerumani na Marekani wameweka msimamo mkali dhidi ya Urusi Jumapili (07.06.2015) mwanzoni mwa mkutano wa Kundi la Mataifa Saba tajiri duniani ambao umegubikwa na mzozo wa Ukraine na Ugiriki.

https://p.dw.com/p/1Fd5S
Viongozi wa Kundi la G/ Elmau (07.06.2015)
Viongozi wa Kundi la G/ Elmau (07.06.2015)Picha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Kansela Angela Merkel alianza siku kwa kumuonyesha ukarimu Rais Barack Obama katika tafrija ya jadi ya jimbo la Bavaria la kubwia pombe na kitafunio cha mkate maalum kwenye bustani huku wakibirudishwa na muziki unaopigwa na wenyeji waliovalia suruali za ngozi.

Lakini baada ya kutabasamu kwenye mwanga wa jua viongozi wote wawili wametowa onyo kali kwa Rais Vladimir Putin wa Urusi juu ya kile Obama alichokisema kuwa ni "uchokozi" wake nchini Ukraine.

Taarifa kutoka Ikulu ya Marekani imesema viongozi hao wamekubali kwamba muda wa vikwazo unapaswa dhahir kufungamanishwa na utekelezaji wa Urusi kikamilifu wa makubaliano ya amani ya Minsk na kuheshimu uhuru wa Ukraine ikimaanisha makubaliano yaliofikiwa katika mji mkuu wa Belarus.

Makaribisho ya kitamaduni na kuonyesha umoja ulioko kati ya Ujerumani na Marekani havikuendana kabisa na msimamo wa viongozi hao kwa Urusi ambao haukujumuishwa kwenye mazungumzo yao.

Msimamo mmoja dhidi ya Urusi

Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Donald Tusk ambaye pia anahudhuria mkutano huo unaofanyika kwenye jengo la ngome ya Elmau eneo la mapumziko likiwa chini ya ulinzi mkali amesema anataka kuyakinisha suala la umoja wa Kundi la G7 kuhusiana na sera za vikwazo dhidi ya Urusi ambapo amesema itaendelea kubakia nje ya kundi hilo kwa kadri itakapokuwa inaendeleza vitendo vyake vya ubabe kwa Ukraine na nchi nyengine.

katika makaribisho ya kitamaduni na wenyeji wa jimbo la Bavaria. (07.06.2015)
Rais Barak Obama wa Marekani katika makaribisho ya kitamaduni na wenyeji wa jimbo la Bavaria. (07.06.2015)Picha: Reuters/H. Hanschke

Viongozi wa Japani na Canada walihakikisha kwamba wanazuru Kiev mji mkuu wa Ukraine wakati wakiwa safarini kuja Ujerumani hapo Jumamosi kuelezea uungaji mkono wao viongozi wa Ukraine wakati vikosi vya serikali vikishambuliana tena na waasi mashariki mwa nchi hiyo,

Obama amesema kabla ya mazungumzo yake na Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron kwamba suala kuu katika mkutano huo "litakuwa ni kusimama kidete dhidi ya uchokozi wa Urusi nchini Ukraine."Francois Hollande wa Ufaransa,Matteo Renzi wa Italia, Stephen Harper wa Canada na Shinzo Abe wa Japani wanahuhuria mkutano huo.

Hofu ya kuvunjika makubaliano Ukraine

Kuzuka upya kwa mapigano mashariki mwa Ukraine hivi karibuni kumesababisha watu 28 kupoteza maisha yao na kuzusha hofu kwamba kupamba moto huko kwa mapigano kutavuruga makubaliano ya kusitisha mapigano yaliopatikana kwa taabu chini ya usimamizi wa Ufaransa na Ujerumani kwa miezi minne.

Rais Barak Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ,Elamau. (07.06.2015)
Rais Barak Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ,Elamau. (07.06.2015)Picha: picture-alliance/AP Photo/Matthias Schrader

Obama bila ya kuitaja kwa jina Ugiriki iliokumbwa na mzozo wa kiuchumi pia amegusia matatizo yanayoendelea kuwepo kati ya Umoja wa Ulaya na Ugiriki ilioelemewa na mzigo wa madeni kwa kutaja kwamba mada za juu katika mkutano huo wa kilele ni uchumi wa dunia ambao unazalisha ajira na kuleta fursa na kuendelea kuufanya Umoja wa Ulaya uwe madhubuti na wenye neema.

Merkel anayatetea mageuzi magumu na kubana matumizi ili Ugiriki iweze kupatiwa mikopo amefanya juhudi za mwisho kuupatia ufumbuzi mzozo huo wa Ugiriki siku chache kabla ya mkutano huu wa Kundi la Mataifa Saba ambapo amekuwa na mashauriano na viongozi wa Shirika la Fedha la KImataifa (IMF) Halmashauri ya Umoja wa Ulaya na Benki Kuu ya Ulaya mjini Berlin.

Suala la Ugiriki linatishia kuugubika mkutano huo wa kilele ambao Merkel alitaraji kulenga kwenye matatizo mengine makuu kuanzia na mabadliko ya tabia nchi na Waislamu wa itikadi kali,haki za wanawake,miradi ya afya kwa wananchi na vita dhidi ya umaskini.

Siku moja baada ya kunadamana dhidi ya kundi hilo la G7 katika maandamano ambayo kwa kiasi kikubwa yalikuwa ya amani waandamanaji kadhaa Jumapili walikuwa wamezinga njia kuelekea kwenye kasri ya ngome ya Elmau unakofanyika mkutano huo jambo ambalo limepelekea waandishi kupelekwa kwa helikopta kwenye eneo la mkutano huo.

Mwandishi : Mohamed Dahman/ AFP/AP

Mhariri : Amina Abubakar