1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 20 ya Mauwaji ya Halaiki Rwanda Magazetini

11 Aprili 2014

Kumbu kumbu za miaka 20 ya mauwaji ya halaiki ya Rwanda,hali katika jamhuri ya Afrika kati na wimbi la wakimbizi waliokwama Libya wakiwa na shabaha ya kuelekea Ulaya ni miongoni mwa mada za Afrika magazetini wiki hii.

https://p.dw.com/p/1BgMi
Rais Paul Kagame akihutubia wakati wa kumbukumbu za miaka 20 ya mauwaji ya halaikiPicha: Reuters

Tuanzie na kumbukumbu za miaka 20 ya mauwaji ya Rwanda,mada iliyochambuliwa na wahariri wa magazeti takriban yote ya Ujerumani wiki hii."Muda wa kuandamwa waasisi wa mauwaji ya halaiki haupiti-Kama si leo ,kesho watakamatwa"ndio kichwa cha maneno cha gazeti la mji mkuu-Die Tageszeitung.Gazeti linazungumzia jinsi vyombo vya sheria nchini Rwanda vinavyoshughulikia kesi dhidi ya wahusika wa mauwaji ya halaiki na kuwaandama katika kila pembe ya dunia wale wote walioyaandaa.Rwanda,miaka 20 baada ya mauwaji ya halaiki bado iko mbioni kuwasaka wahalifu na kuwafikisha mahakamani linaandika gazeti la Die Tageszeitung linalozitja juhudi hizo kuwa changamoto kubwa kabisa za kisheria kuwahi kushuhudiwa ulimwenguni.Kesi zaidi ya milioni moja na laki mbili zimeshuhughulikiwa na mahakama ya kienyeji Gacaca kuanzia mwaka 2004 hadi 2012.Gazeti la Die Tageszeitung linazungumzia lawama na ila zilizotolewa dhidi ya mahakama hizo za kienyeji hata hivyo gazeti linaungama bila ya Gacaca pengine juhudi za kuwaandama mahakamani wahalifu zingedumu miaka 100.Gacaca zilifunga utaratibu wa kusikliliza kesi mwaka 2010 na kukabidhi vyombo vya kawaida vya sheria vya Rwanda.Hata mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa vita nchini Rwanda iliyoko mjini Arusha nchini Tanzania inaelekea kukamilisha hivi sasa kesi zake,watuhumiwa wote waliosalia watakuwa wanashughulikuwa hivi sasa na vyombo vya sheria vya Rwanda.Bado linaandika Die Tageszeitung,mkuu wa kitivo cha ukaguzi kataika ofisi ya mwendesha mashtaka mkuu Jean Bosco Siboyintore anawasaka watuhumiwa katika kila pembe ya dunia.Ofisi kwake limetundikwa bango la shirika la polisi ya kimataifa Interpol lenye picha za watuhumiwa hao wanaosakwa kwa waranti wa kimataifa.Si rahisi kuwagundua,wengi wao wamebadilisha majina na wanaishi kama wakimbizi nchi za nje,die Tageszeitung limemnukuu Siboyintore akisema.

Ufa unazidi kupanuka katika Uhusiano kati ya Rwanda na Ufaransa

Frankfurter Allgemeine pia limezungumzia kumbukumbu za miaka 20 ya mauwaji ya halaiki nchini Rwanda.Gazeti limemulika zaidi lakini uhusiano uliozidi kuchafuka kati ya Rwanda na Ufaransa."Miaka 20 baada ya mauwaji ya halaiki nchini Rwanda,pengo kati ya Kigali na Paris linazidi kupanuka-chanzo ni nafasi ya Ufaransa,zamani na leo barani Afrika linaandika Frankfurter Allgemeine .Ufaransa ilitaka kuwakumbuka kwa hadhi wahanga wa mauwaji lakini mambo yalibadilika limeandika Frankfurter Allgmeine lililokumbusha tuhuma za rais Paul Kagame dhidi ya Ufaransa zilizopelekea ujumbe wa Ufaransa uliokuwa uongozwe na waziri wa sheria Christiane Taubira kuvunja safari na balozi wa Ufaransa mjini Kigali kukataliwa ruhusa na Kigali ya kushiriki katika kumbu kumbu hizo.

Badala ya MISCA,sasa MINUSCA watawajibika Jamhuri ya Afrika Kati

Hali katika jamhuri ya Afrika kati pia ilimulikwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani wiki hii.Gazeti la Neues Deutschland limezungumzia matumizi ya nguvu yanayoendelea kati ya makundi ya wanamgambo wa kikristo na kiislam.Pekee wiki hii inayomalizika watu zaidi ya 40 wameuwawa.Rais wa mpito Catherine Samba-Panza hajui afanye nini.Matumaini yake na yale ya wananchi walio wengi yameelekezwa Umoja wa mataifa ulioamua, linaandika Neues Deutschland kutuma wanajeshi 12 elfu kushika nafasi ya wanajeshi elfu sita wa Afrika waliokuwa wakitumikia kikosi cha MISCA.Kikosi hicho kipya kwa jina MINUSCA kitaanza kufanya kazi septemba 15 ijayo.

Catherine Samba-Panza
Rais wa mpito wa jamhuri ya Afrika Kati bibi Catherine Samba-PanzaPicha: Reuters

Wimbi la Wakimbizi katika Bahari ya Kati

Ripoti yetu ya mwisho katika ukurasa huu wa Afrika katika magazeti ya Ujerumani wiki hii inatufikisha Libya ambako kwa mujibu wa gazeti la Der Tagesspiegel zaidi ya watu elfu nne wameokolewa katika bahari ya kati wakiwa njiani kuelekea Italia.Gazeti hilo limenukuu ripoti ya gazeti la Italia Repubblica inayosema wengi wa watu hao wanatokea Eritrea,Ethiopia,Syria na maeneo ya utawala wa ndani wa Palastina.Der Tagesspiegel linakumbusha tangu mwaka huu ulipoanza zaidi ya waakimbizi 15 elfu wameokolewa.Linajiuliza nani ajuaye wangapi wengine wanapanga kujitosa katika bahari ya kati kabla ya mwaka huu kumalizika.Gazeti linamalizia kwa kuandika wakaimbizi laki sita wamekwama nchini Libya-wanasubiri upenu wa kujitosa kuelekea Ulaya.

Italiens Marine rettet in kurzer Zeit mehr als 1000 Flüchtlinge 8.4.2014
Wakimbizi waliookolewa hivi karibuni karibu na fukwe za ItaliaPicha: Reuters

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/BASIS/PRESSER/ALL/Presse

Mhariri:Yusuf Saumu