1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel akosoa mpango wa Israeli

6 Desemba 2012

Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel ameukosoa mpango wa Israeli wa kujenga makaazi mapya ya walowezi katika eneo la Jerusalem Mashariki na kuitaka kuendeleza juhudi za kupatikana ufumbuzi wa kuwepo mataifa mawili.

https://p.dw.com/p/16wvQ
Benjamin Netanyahu na Angela Merkel
Benjamin Netanyahu na Angela MerkelPicha: dapd

Akizungumza leo katika mkutano na waandishi wa habari na Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu mjini Berlin, Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema kwa kawaida Ujerumani imekuwa ni miongoni mwa mshirika mkubwa wa Israeli, lakini mpango wa kujenga makaazi 3,000 ya walowezi katika eneo muhimu la Ukingo wa Magharibi, umesababisha upinzani wa kimataifa na kuifanya Ujerumani kuukosoa wazi mpango huo. Kansela Merkel amebainisha kwamba mazungumzo ya kutafuta ufumbuzi wa kuwepo mataifa mawili lazima yaendelee na kwamba hatua zinazochukuliwa na upande mmoja hazina budi kuepukwa. Amerudia kuelezea dhamira yake kuhusu usalama wa Israeli.

Netanyahu asikitishwa na hatua ya Ujerumani

Kwa upande wake Netanyahu ameelezea kusikitishwa na hatua ya Ujerumani kutopiga kura katika Hadhara kuu ya Umoja wa Mataifa, ingawa amesema kwamba ana uhakika Ujerumani inaunga mkono ustawi wa Israeli. Amefafanua kuwa bado ana amini anaungwa mkono na Ulaya, hata baada ya baadhi ya nchi za Umoja huo kuwahoji mabalozi wa Israeli walioko katika nchi hizo ikiwa ni katika kupinga mpango huo wa ujenzi wa makaazi mapya ya walowezi kwenye Ukingo wa Magharibi. Amesema hadhani kama wameipoteza Ulaya, ingawa kuna mtazamo tofauti barani humo kuhusu suala la ujenzi wa makaazi mapya. Netanyahu amesema Ulaya imeuelewa vibaya mgogoro wa Mashariki ya Kati na kudhani kuwa ni kuhusu suala la makaazi peke yake, akisisitiza kuwa hilo siyo chimbuko la matatizo na kwamba matatizo yalianza baada ya mwaka 1967.

Viongozi wa Ujerumani na Israeli
Viongozi wa Ujerumani na IsraeliPicha: Reuters

Israeli yafikia uamuzi huo baada ya kura ya UN wiki iliyopita

Hatua ya Israeli kutangaza kujenga makaazi mapya ya walowezi imefikiwa baada ya wiki iliyopita hadhara kuu ya Umoja wa Mataifa kupiga kura ya kuipandisha hadhi Palestina kuwa mtazamaji asiyekuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa. Aidha, Wapalestina wanasema kuwa mpango huo wa Israeli katika ardhi ambayo wanaipigania kuwa taifa lao, unaweza ukaugawa Ukingo wa Magharibi na kujitenga kutoka Jerusalem, ambao utakuwa mji wao mkuu wa baadae. Mbali na mkutano wa Merkel na Netanyahu, ilifanyika pia mikutano iliyohusisha mawaziri saba wa Israeli na mawaziri kumi wa Ujerumani ambapo pamoja na mambo mengine wamezungumzia miradi ya pamoja katika sekta ya sayansi na elimu.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/RTRE,DPA
Mhariri:Yusuf Saumu