1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matukio makuu michezoni 2012

31 Desemba 2012

Haya ni baadhi ya matukio muhimu yaliyotokea katika viwanja vya michezo katika mwaka wa 2012, ikiwa ni pamoja na kandanda, michezo ya Olimpiki jijini London, riadha na kadhalika

https://p.dw.com/p/17BcL
LONDON, ENGLAND - JULY 27: Fireworks ignite over the Olympic Stadium during the Opening Ceremony for the London 2012 Olympic Games on July 27, 2012 at Olympic Park in London, England. (Photo by Jamie Squire/Getty Images)
Bildergalerie - Sport Highlights 2012Picha: Getty Images

Tunaanza uchambuzi wetu katika viwanja vya kandanda ambapo, ushindi wa tatu mfululizo wa Uhispania, katika kinyang'anyiro kikuu na umaahiri wa kibinafsi wa ufungaji mabao wake Muargentina Lionel Messi ni matukio yatakayokumbukwa katika madaftari ya mwaka wa 2012. Lakini mwaka huo pia ulikumbwa na mikasa ya vifo vya Misri na Uholanzi na wasiwasi wa ongezeko la matukio ya kibaguzi katika kandanda barani Ulaya.

Ni mwaka ambao pia ulimwengu wa soka ulibadilika kutoka enzi za karne ya 19, na kuingia katika karne ya 21 wakati teknolojia ya kubainisha iwapo mpira umevuka mstari kwenye lango ilipoidhinishwa na shirikisho la soka ulimwenguni FIFA. Mbinu hii ilitumiwa rasmi kwa mara ya kwanza katika mashindano ya fainali za Klabu bingwa ulimwenguni nchini Japan. Katika dimba hilo, klabu ya Corinthians kutoka Brazil iliibuka kidedea kama klabu bora ulimwenguni, taji ambalo natumai kila mmoja wetu atakubali kwamba linapaswa kuwaendea Barcelona wa Uhispania.

Lakini mojawapo ya mishangao mikubwa iliyotokea katika mwaka huu, Barcelona walishindwa kutwaa kombe la Ligi ya Mabingwa Ulaya- UEFA Champions League, ambalo lilionekana kuwa lao, kabla ya kuduwazwa na Chelsea katika nusu fainali, wakati Messi alipodhihirisha kuwa kumbe yeye pia ni binaadamuu na wala siyo kiumbe kilichozaliwa nje ya dunia, aliposhindwa kufunga penalti. Hata hivyo Messi alimaliza mwaka kwa kufunga magoli 91, ikiwa ni rekodi mpya kabisa ulimwenguni, baada ya kuifuta ile iliyowekwa na mshambuliaji wa zamani wa Ujerumani Gerd Mueller iliyodumu miaka 40.

Mshambuliaji Lionel Messi mchezaji bora ulimwenguni
mshambuliaji Lionel Messi mchezaji bora ulimwenguniPicha: AFP/Getty Images

Chelsea ambao walimaliza Premier League ya England wakiwa katika nafasi ya sita mwezi Mei, walienda moja kwa moja na kunyakua taji la Champions league katika fainali mjini Munich. Baada ya kufutiliwa mbali kabisa na vyombo vya habari vya Ulaya kabla ya kucheza dhidi ya Barca, waliwaduwaza tena wakosoaji kwa kuwazaba Bayern Munich kwa mikwaju ya Penalti katika uwanja wao wa Allianz Arena na kuwa klabu ya kwanza ya London kunyanua kombe hilo la Ulaya katika historia yake ya miaka 57.

Kando na kushinda pia kombe la FA, miezi sita baadaye, Roberto Di Matteo akapigwa kalamu na mmliki bwenyenye Roman Abramovich kabla ya klabu hiyo kuwa bingwa mtetezi wa kwanza kuondolewa katika dimba la Champions league. Aidha kukawa na matukio ya John Terry kuhusika katika madai ya kumtlea mchezaji matamshi ya kibaguzi. Uhispania waliwazaba Italia magoli manne kwa sifuri katika fainali ya kombe la Mataifa ya Ulaya, UEFA EURO 2012, yaliyoandaliwa Ukraine na Poland. Real Madrid kisha wakawapiku Barca katika La Liga, lakini msimu huu Barca wamerejea tena kileleni mbele kabisa ya Real.

Katika mikasa mibaya zaidi, nchini Misri, ikumbukwe kwamba mnamo Februari mosi mjini Port Said, zaidi ya mashambiki wa Misri 70 waliuawa kufuatia rabsha zilizozuka baada ya mchuano wa ligi kati ya al-Masry ya Port Said na al-Ahly ya Cairo, huku wafuasi wengi, polisi na maafisa wengine kudungwa visu hadi kufa. Ghasia hizo zilitokana na hofu ya kisiasa nchini humo na kusababisha Ligi kuu ya Kandanda Misri kusimamishwa.

Mji wa Port Said nchini Misri ulishuhudia ghasia mbaya zaidi
Mji wa Port Said nchini Misri ulishuhudia ghasia mbaya zaidiPicha: AP

Lakini kuna muujiza uliotokea baada ya aliyekuwa mchezaji wa Bolton Fabrice Muamba, alipozirai uwanjani wakati wa mchuano wa Premier League dhidi ya Tottenham Hotsour uwanjani White Heart Lane. Madaktari walisema Muamba alikufa kwa dakika 78, na kuutaja kurejesha fahamu kwake kuwa muujiza mkubwa. Tukio hilo limemfanya Muamba kuwachana na mambo ya soka kutokana na ushauri wa madkatari. Aidha katika matukio mengine mwaka ya mwaka, Zambia waliibuka kidedea katika dimba la mataifa ya Afrika lililoandaliwa Gabon na Guinea ya Ikweta. Chipolopolo jinsi wanavyohamika, waliwalaza Cote d'Ivoire waliokuwa wamepigiwa upatu zaidi kulishinda kombe hilo, magoli 8 – 7 kupitia mikwaju ya penalti baada ya mchuano kukamilika sare ya bila kufungana katika muda wa ziada.

Kule England, Manchester City waliwazidi nguvu na kuwapokonya Manchester United taji la Premier League kwa wingi wa magoli, ushindi ambao ulipatikana katika sekunde za mwisho mwisho, ikiwa ni ushindi wao wa kwanza katika miaka 44. Nchini Ujerumani katika Bundesliga, Borussia Dortmund walinyakua taji la Bundesliga kwa mara ya pili mfululizo. Ushindi huo ulithibitisha kuibuka kwa Borusssia Dortmund kama hasimu mkuu wa klabu ya Bayern Munich katika soka ya ligi kuu Ujerumani Bundesliga.

Borussia Dortmund mabingwa mara mbili wa Ujerumani
Borussia Dortmund mabingwa mara mbili wa UjerumaniPicha: AFP/Getty Images

Dortmund ilikuwa timu ya kwanza kando na Bayern, kuhifadhi taji la Bundesliga tangu ilipofanya hivyo miaka 16 iliyopita, na kumaliza desturi ya Bayern ya kushinda taji la ligi karibu kila msimu wa pili tangu mwaka wa 1996. Dortmund ilinyakua taji lake la nane la ligi ya Ujerumani wakati ilipoendeleza rekodi ya Bundesliga ya kutoshindwa katika mechi 26 mfululizo. Na walimaliza msimu kwa kuwa mabingwa mara mbili, yaani Bundesliga, na DFB Pokal. Hata hivyo kando na kufanya vyema katika jukwaa la Ulaya, Champions League, Dortmund wanaonekana kuwa wamesalimisha taji kwa Bayern ambao wamemaliza nusu ya kwanza ya msimu wakipepea kileleni na hawaonekani tena kukubali kuangusha pointi, ligi itakapoanza baada ya mapumziko ya msimu wa baridi

Michezo ya Olimpiki London 2012

Uingereza ilitumia takribani kiasi cha pauni bilioni tisa kuandaa viwanja vya kuvutia kwa ajili ya michezo ya Olimpiki ya mwaka wa 2012, ambako mashabiki waliburudishwa kote jijini London kutokana na maandalizi ya michezo hiyo. Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron alisema baada ya mashindano hayo kwamba, wameuonyesha ulimwengu kile walicho nacho, na kujikumbusha wao kile wanachoweza kufanya.

Michezo ya Olimpiki 2012 ilidhihirisha jukwaa maalum kwa mwanariadha wa kasi zaidi ulimwenguni Usain Bolt, aliyeibuka kuwa mtu wa kwanza ulimwenguni kutetea mataji yake ya mbio z mita 100 na 200. Katika vidimbwi vya kuogelea. Mwogeleaji wa Marekani Michael Phelps alivunja rekodi yakuwa mwana olimpiki maarufu zaidi kwa kunyakua jumla ya medali 22, zikiwemo 18 za dhahabu. Phelps alitumia mashindano hayo kuwa yake ya mwisho katika taaluma yake na hapo katangaza kustaafu kutoka mchezo huo. Marekani ilimaliza kileleni katika mashindano ya Olimpiki jijini London, baada ya kumaliza nyuma ya China katika mashindano ya Beijing. Marekani walizoa jumla ya medali 46 za dhahabu, kati ya jumla ya medai 104. China ilinyakua dhahabu 38 kati ya jumla ya medali 87 katika nafasi ya pili. Wenyeji wa michezo hiyo walimaliza katika nafasi ya tatu mbele ya Urusi wakiwa na dhahabu 29. mwanariadha wa Uingereza mzaliwa wa Somalia o Farah aliibuka shujaa baada ya kunyakuwa dhahabu mbili katika mbio za mita 5,000 na 10,000. Mkenya David Rudisha alivunja rekodi ya ulimwengu ya mita 800 na kunyakua dhahabu kwa kutumia muda wa dakika moja, sekunde 40 nukta 91 ushindi huo ulimfanya Afisa mkuu wa michezo ya Olimpiki London Sebastian Coe kuutaja kama ushindi maarufu katika mashindano hayo ya London 2012.

LONDON, ENGLAND - JULY 27: Fireworks ignite over the Olympic Stadium during the Opening Ceremony for the London 2012 Olympic Games on July 27, 2012 at Olympic Park in London, England. (Photo by Jamie Squire/Getty Images)
Bildergalerie - Sport Highlights 2012Picha: Getty Images

Katika kandanda upande wa wanawake, Marekani iliwapiku Japan katika fainali magoli mawili kwa moja, na kunyakua dhahabu ya tatu mfululizo katika olimpiki. Na kwa upande wa wanaume, washindi mara tano wa Olimpiki Brazil, waliwachwa kinywa wazi baada ya kuzabwa na Mexico. Andy Murray hatimaye aliweza kupata ushindi wa Wimbledon katika fainali ya kuvutia dhidi ya Roger Ferderer. Katika mpira wa kikapu miamba wa Marekani katika NBA waliwanyamzisha Uhispania katika fainali na kuhifadhi taji lao la olimpiki

Sebastian Vettel atawala Formula One

Katika mbio za magari ya Formula One, Sebastian Vettel alishinda kwa mara ya tatu mfululizo na kuisaidia timu yake ya Red Bull kunyakuwa taji la tatu mfululizo la ujenzi bora, lakini Mjerumani huyo chipukizi hakupata ushindi huo kibinafsi katika mwaka wa 2012. Wakati akiponyoka na taji la mwaka wa 2011, Vettel alilazimika kupunguza pengo la pointi dhidi ya kiongozi Fernando Alonso wa Ferrari na kuwa mtu wa tatu pekee katika mchezo huo kushinda mataji kwa miaka mitatu mfululizo, na kujiunga na Mjerumani Michael Schumacher na Juan Manuel Fangio. Wakati huo huo dereva wa muda mrefu Michael Schumacher alitangaza kustaafu kwake kabisa kutoka mchezo huo.

Sebastian Vettel aliipeperusha bendera ya Red Bull
Sebastian Vettel aliipeperusha bendera ya Red BullPicha: Reuters

Lance Armstrong apokonywa mataji

Bila shaka tukio jingine kuu lililotokea katika mwaka wa 2012, na ambalo litakumbukwa na wengi ni sakata iliyomkumba mwendeshaji basikeli maarufu Lance Armstong. Sakata hiyo iliwacha pengon kubwa katika madaftari ya kumbukumbu katika mchezo wa uendeshaji baisikeli, na kuchafua kabisa hadhi ya mchezo huo. Armstrong alipigwa marufuku ya maisha na kupokonywa mataji yake yote saba ya mashindano ya Tour de France baada ya shirika la Marekani la kupambana na matumizi ya dawa za kusisimua misuli – USADA kufichua kile ilichosema kuwa ni mbinu yenye ujuzi wa hali ya juu ya matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku kuwahi kupatikana. Hata hivyo Armstrong alitangaza kuwa hataweza tena kupinga madai hayo ya matumizi ya dawa haramu, baada ya jaji kukataa kuisimamisha shughuli hiyo ya kumchunguza. Mwendeshaji baiskeli huyo Mmarekani alishinda mataji hayo saba ya Tour de France kutoka mwaka wa 1999-2005. Armstrong alidaiwa kuchukua usukani kabisa ambapo vyumba vya hoteli vilibadilishwa kuwa hifadhi za damu, madaktari wakalipwa nao waendeshaji baiskeli wakaonywa dhidi ya kufanya vipimo vya mapema kabla ya mashindano. Lance Armstrong ambaye ni mwathiriwa wa saratani, aliiuduwaza ulimwengu wa undeshaji baiskeli kutokana na umahiri wake.

Klitschko mabingwa wa ndondi

Katika ndondi shujaa wa ndondi wa Ufilipino Manny Pacquiao ametiririkwa na macho kwenye televisheni ya taifa akisema ameifedhehesha nchi baada ya kurambishwa sakafuni kwa njia ya knock out na hasimu wake kutoka Mexico Juan Manuel Marquez. Pacquiao amekiri kushindwa, akisema hiyo ni kazi yake, lakini ana machungu kuona jinsi Ufilipino ilivyohuzunika kutokana na kichapo hicho. Mkewe alitoa hotuba akimtaka mwanabondia huyo aliyekuwa bingwa mara nane wa ulimwengu, kuzitundikla glovu zake. Pacquiao hajazungumzia lolote kuhusu miito hiyo ya kumtaka astaafu. Amesema aliingia ulingoni jana Jumapili akiwa na matumaini makubwa ya kumzaba Marquez. Lakini hiyo ndiyo hali ya mchezo, unaweza kushinda au kushindwa. Ameongeza kwamba analenga kupigana tena hivi karibuni.

Kaka wawili, Wladmir na Vitali Klitschko wametawala ndondi
Kaka wawili, Wladmir na Vitali Klitschko wametawala ndondiPicha: dapd

Tukisalia na mambo ya ndondi, ni kwamba suali kubwa linalosalia kuulizwa na mashabiki katika mwaka wa 2013, ni Nani anayeweza kuwasimamisha ndugu wawili Klitschko katika kitengo cha uzani wa heavyweight? Kwa sasa hakuonekani mpinzani anayeweza kufanya hivyo.

Baada ya kushikilia mataji ya WBA, IBF, IBO na WBO kwa miezoi 18 iliyopita, Wladmir Klitschko alipata ushindi wake wa 69 katika taaluma yake mnamo mwezi Novemba wakati alipopata ushindi kupitia wingi wa pointi dhidi ya Mariusz Wach wa Poland. Kama kawaida kulikuwa na uvumi kuhusu pigani baina ya pengine Witali, bingwa wa WBC au Wladmir dhidi ya David Haye wa Uingeerza, ambaye alirudi tena ulingoni baada ya kustaafu na kumrambisha sakafuni kwa njia ya knock put David Chisora mwezi Julai.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters/dpa/afp/Ap

mhariri: Josephat Charo